27 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Chadema yahofia kuhujumiwa na Takukuru

Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimesema kinashangazwa na mwenendo wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuhusu uchunguzi inaoufanya kuhusu chama hicho kinyume na sheria.

Kutokana na hilo, kimeitaka Takukuru kueleza rasmi makosa ya chama hicho na si kuchukua kauli za kisiasa na kufanyia uchunguzi.

Mwishoni mwa Mei mwaka huu, Takukuru ilisema imeanza kuchunguza tuhuma za matumizi mabaya ya fedha ya Chadema, ikiwemo wabunge wa chama hicho kukatwa mishahara yao.

Baadaye wabunge 69 na viongozi wengine wa chama hicho pamoja na waliowahi kuhudumu kupitia chama hicho, walihojiwa na Takukuru.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika alisema pamoja na kwamba walitoa ushirikiano tangu mwanzo wa nyaraka mbalimbali za matumizi ya fedha na wabunge kuhojiwa, lakini taasisi hiyo imewaandikia barua nyingine mbili.

Mnyika alisema katika barua hizo mbili Takukuru inawataka kuwasilisha nyaraka zingine za vikao na mipango ya chama kuanzia mwaka 2014-2020.

“Sasa barua yao hii ni wazi kwamba Takukuru imeingia kutekeleza kauli iliyowahi kutolewa na Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Bashiru Ally kuwa watatumia vyombo vya dola kubaki madarakani,” alisema Mnyika.

Alisema wanashangazwa kwa mwenendo huo wa Takukuru kwa sababu katika barua zao hakuna uchunguzi wa kosa kama vifungu vya sheria vinavyoelekeza ikiwa kuna kosa.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge Kibamba, alisema kutokana na hali hiyo, wameiandikia barua Takukuru ambayo imejibu kile walichotaka. 

“Sasa tumewajibu na tumewasilisha barua yetu leo (jana) kuwa watujulishe rasmi kwa mujibu wa sheria kuhusu kile wanachokichunguza ili tuendelee kuwapa ushirikiano, tunataka watupe majibu rasmi na kwenye barua tumewaeleza bayana kuwa tunaona jambo hili lina mwelekeo wa kisiasa wa kuokoteza makosa.

“Pia tumeitaka Takukuru izingatie kwamba hadi sasa haijaeleza kosa au makosa jambo ambalo Chadema tulishaweleza awali.

“Hadi sasa Chadema imeshatoa nyaraka na michango ya wabunge, viongozi na wabunge wamefanyiwa mahojiano kuhusu fedha za wabunge, pia tumewaeleza wigo wa hicho inachodaiwa kuwa uchunguzi hauonyeshi ukomo wala makosa,” alisema Mnyika.

Aidha alisema kutokana na mazingira ya kisiasa hapa nchini na kwa kuwa wako kwenye maandalizi ya Uchaguzi Mkuu, wanapata wakati mgumu kuendelea kutoa ushirikiano bila kufahamu ukomo wa uchunguzi au jambo au kosa mahususi ambalo wanachunguzwa.

“Chadema inatatizwa zaidi kwa Takukuru kutumia kauli za kisiasa zinazotolewa na watu na sasa tunaitaka Takukuru iongozwe kwa mujibu wa sheria,” alisema Mnyika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles