27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

CCM IKO IMARA NA MAGUFULI HAJALETA HOFU

magufuliccm

Na Charles Charles

UPOTOSHAJI unaofanywa na baadhi ya vyombo vya habari nchini, umeendelea tena kwa gazeti moja linalokiunga mkono chama kimoja cha upinzani, kuchapisha habari yenye kichwa kinachosema “JPM azusha hofu mpya CCM” na kudai ifuatavyo:

(1) Kwamba mabadiliko makubwa ya kimuundo yaliyotangazwa siku chache zilizopita na Chama Cha Mapinduzi (CCM), yamezusha hofu kwa makada wake kuwa mwanzo wa kukiua badala ya kukiimarisha.

Tangu kumalizika kwa vikao vya Kamati Kuu na hatimaye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Jumanne Desemba 13, 2016 hadi sasa hakuna mwanachama, kiongozi wala mfuasi yeyote wa CCM aliyelalamika, kuhoji au kunung’unukia mabadiliko yoyote yaliyopitishwa na vikao hivyo.

Badala yake, madai ya gazeti hilo ambalo limejipambanua wazi kuwa linakisemea, kukitumikia na kutekeleza matakwa yote ya chama hicho cha upinzani huku likiwa liko huru ni habari za kufikirika kichwani, zile ambazo licha ya kutungiwa mezani pia zinaweza kuitwa kuwa za ni kuokoteza barabarani.

 

(2) Kwamba mabadiliko ya kupunguza Wajumbe wa Kamati Kuu kutoka 34 na kubaki 24 na Wajumbe wa NEC kutoka 388 na kubaki 158 yanalenga kukifanya chama hicho kuwa cha wachache katika ngazi za uamuzi, hatua ambayo itakuwa na athari zaidi kwa CCM.

UKWELI ULIVYO

Vikao vyote vya CCM katika ngazi zote ni vya uwakilishi, hivyo idadi ya watu siyo hoja na haina msingi wowote.

Ndiyo maana kwa mfano Kamati za Usalama na Maadili katika ngazi zote za matawi, kata, wilaya mpaka mikoa zinaundwa na wajumbe watano tu.

Kama watu watano wanaweza kuwawakilisha wana CCM wote katika mkoa mzima kwa mfano, inawezekanaje kwa wawakilishi 158 kwa mikoa 31 waonekane wachache?

Lakini pia, hivi watu 388 wanapokutana mahali hicho kinakuwa kikao au mkutano wa hadhara ambao hata mijadala yake inaweza isifanyike kwa usahihi?

Hivi inawezekana kwa watu wote hao kuchangia kwenye kikao cha siku moja au mbili tu?

 

(3) Madai kwamba hatua ya kila wilaya kuwa na Mjumbe wa NEC inawafanya wana CCM waone chama kimepelekwa mkononi mwao, na pia inakuwa rahisi kwake kuwapelekea wenzake mambo waliyokubaliana kwenye vikao.

UKWELI ULIVYO

Nafasi za Wajumbe wa NEC wanaowakilisha wilaya ambazo sasa zinaondolewa hazikuwahi kuwepo katika historia ya TANU, ASP wala CCM yenyewe tokea ianzishwe mwaka 1977 hadi zilipoanzishwa miaka minne iliyopita, yaani mwaka 2012 tu.

Hivi kama hazikuwepo kwa miaka yote 23 ya uhai wa TANU, miaka yote 20 ya uhai wa ASP na miaka 35 ya CCM na chama kilikuwa kinafanya vizuri katika malengo yake ya kisiasa, hivi uwepo wao wa miaka hiyo umeleta tija gani ambayo wakiondolewa itakuwa hasara?

Kuhusu madai kwamba wanapotoka kwenye vikao vya NEC walikuwa wanawapelekea wanachama kile kilichoamuliwa pia ni hisia za kufikirika vichwani mwa watu wasiohusika na chochote kile kwa CCM.

Kazi ya kuwapelekea wana CCM maamuzi mbalimbali ya NEC siyo ya Wajumbe wa NEC ila inafanywa na Katibu Mkuu wa CCM kupitia kwa makatibu wa chama hicho wa mikoa, wilaya, majimbo (kwa Zanzibar), kata, matawi na hatimaye wa mashina.

Hao ndio huifanya kazi hiyo kwa kuzingatia Ibara za 25(a), 44(2)(a) – (c), 58(2)(a) – (c), 72(2)(a) – (c), 86(2)(a) – (c) na 100(2)(a) – (c) za Katiba ya CCM ya Mwaka 1977 Toleo la 2012 inayotumika sasa.

(5)Kwamba kuondolewa kwa Wajumbe wa NEC wanaowakilisha wilaya kutaiweka CCM katika hali ngumu hasa wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji wa mwaka 2019.

Inaelezwa kuwa hiyo itatokana na kwamba katika uchaguzi kama huo mwaka 2014, vyama vya upinzani vilipata wenyeviti wengi wa vijiji na mitaa, hivyo kutokuwepo kwa wajumbe hao vinaweza kufanya vizuri zaidi.

Inawezekana ikawa ni chini ya asilimia tano tu ya wajumbe wote wa NEC wanaowakilisha wilaya zao walioshiriki kwa njia moja ama nyingine, kuwafanyia kampeni wagombea uenyekiti ama ujumbe wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji wa mwaka 2014.

Mwandishi wa makala haya ni Katibu wa Habari wa Katibu Mkuu wa CCM

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles