23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Canada yaahidi neema Tanzania

Na Farida Ramadhani na Peter Haule, WFM Dodoma

Serikali ya Canada imeahidi kuisaidia Tanzania katika kuimarisha sekta ya afya, elimu na mazingira kutokana na ufanisi wa usimamizi wa fedha za miradi inayotekelezwa nchini kwa ushirikiano wa serikali hiyo.

Hayo yamebainishwa jijini Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba wakati wa mkutano wake na Balozi wa Canada Tanzania, Pamela O’Donnell, ulioangazia ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

Dk. Nchemba amesema kuwa sekta ambazo Serikali ya Canada imeahidi kuzisaidia zina umuhimu katika maendeleo ya nchi.

Amesema Tanzania na Canada zitaanzisha mazungumzo mapya ya namna ya kuendeleza programu za maendeleo zilizokuwa zikifadhiliwa na  nchi hiyo baada ya progamu iliyokuwepo kumaliza muda wake Juni, 2021.

Aidha amesema Canada imeisaidia Tanzania katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo ya sekta ya madini, elimu, afya na utawala bora yenye thamani ya dola za Kimarekani  bilioni 2.39 tangu Tanzania ilipopata uhuru.

Waziri huyo amemshukuru balozi huyo  kwa kutambua juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi bora unaotambuliwa duniani kwa kuimarisha uhusiano wa kimataifa.

Kwa upande wake Balozi O’Donnell, amesema kuna mafanikio makubwa ambayo yamepatikana katika miradi mbalimbali iliyotekelezwa nchini Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Canada hususani katika Mfuko wa Afya na Elimu, ambapo fedha zilizotolewa zimetumika kikamilifu katika masuala yaliyokusudiwa.

“Kutokana na jitihada za Serikali katika kutekeleza miradi, tunaona kuna fursa ya kuendeleza ushirikiano katika masuala mbalimbali ikiwemo elimu, afya na kuwajengea uwezo wanawake”, amesema Balozi  huyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles