31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

CAMEROON YASHINDWA KUFUZU KOMBE LA DUNIA

YAOUNDE, CAMEROON

HATIMAYE mabingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika, Cameroon, wameshindwa kuonesha ubora wao na kujikuta wakitolewa katika michuano ya kufuzu Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi.

Mabingwa hao walipewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri kwenye michezo hiyo na kufuzu Kombe la Dunia kutokana na uwezo wao waliouonesha kwenye michuano ya Mataifa ya Afrika, huku ikiwatumia wachezaji wengi vijana, lakini wamekutana na ushindani wa hali ya juu na kutolewa nje.

Juzi walishuka dimbani mjini Yaounde na kulazimishwa kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Nigeria, jambo ambalo limewafanya washindwe kufuzu Kombe la Dunia kwa kuwa sare hiyo wanakuwa na jumla ya pointi 3 baada ya kucheza michezo minne sawa na Nigeria wenye pointi 10, kabla ya mchezo wa jana kati ya Zambia dhidi ya Algeria kwenye kundi hilo B.

Nigeria walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya 30 lililowekwa wavuni na nyota wao, Moses Simon, lakini Cameroon waliweza kusawazisha katika dakika ya 75 kupitia kwa mchezaji wake Vincent Aboubakar.

Dakika 15 za mwisho, Cameroon walionekana kupambana ili kutafuta bao la ushindi lakini mlinda mlango wa Nigeria, Ikechukwu Ezenwa, alionesha kiwango cha hali ya juu kwa kuokoa mipira miwili ya hatari iliyopigwa na Arnaud Djoum na Collins Fai.

Cameroon imekuwa timu ya kwanza kutoka Afrika kushindwa kufuzu Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi, huku ikiwa chini ya kocha wao Hugo Broos.

Kocha huyo amesema, japokuwa ameshindwa kufuzu, lakini bado ataendelea kuwa kocha wa timu hiyo na kupambana kuhakikisha anatwaa tena taji la Kombe la Mataifa ya Afrika msimu ujao.

“Bado ninahitaji kuendelea kuwa hapa, sina mpango wa kujiuzulu, lengo langu ni kuhakikisha ninashinda tena taji la Mataifa ya Afrika kwa mara ya pili mwaka 2019 kwenye ardhi ya nyumbani. Sijatangaza kujiuzulu kwa kuwa mimi si miongoni mwa makocha ambao wanaachana na timu baada ya kufanya vibaya,” alisema.

Afrika kuna makundi matano, hivyo vinara wa makundi hayo watajihakikishia wanakata tiketi ya kushiriki michuano hiyo, timu ya Tunisia, Nigeria, Ivory Coast, Burkina Faso na Uganda zinaongoza kwenye makundi hayo kabla ya michezo ya jana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles