24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Byabato: TANESCO malizeni kulipa fidia Simiyu kabla ya Machi mwaka huu

Na Zuena Msuya, Simiyu

Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato, ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kukamilisha haraka zoezi la kuwalipa fidia wananchi waliobaki ambao wamepisha Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme  kilichopo Kijiji cha Imalilo wilayani Bariadi mkoani Simiyu, kabla ya mwezi Machi mwaka huu.

Naibu Waziri wa Nishati,Wakili Stephen Byabato (aliyenyoosha mkono) akiwaonyesha kitu wasimamizi wa ujenzi wa kituo wakiwemo Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), wakati wa ziara ya kukagua eneo litakalojengwa Kituo cha Kupoza Umeme kilichopo Kijiji cha Imalilo wilayani Bariadi mkoani Simiyu, Februari 24,2021.

Wakili Byabato alitoa maagizo hayo, Februari 24, 2021 baaada ya kufanya ziara ya kutembelea eneo hilo linalotarajiwa kuanza kujengwa kituo hicho mwezi Julai, mwaka huu, na kuzungumza na baadhi ya wananchi ambao bado hawajalipwa fidia kutokana na changamoto mbalimbali kujitokeza.

Alitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na kutofautiana kwa majina yaliyoandikwa katika vitambulisho vyao, nyaraka na hundi, zilizokuwa zikitumika kuwalipa fedha za fidia.

Aliweka wazi kuwa ni wananchi watano (5) tu kati ya Arobaini na Watano (45) waliopaswa kulipwa fidia bado hawajalipwa, Arobaini (40) tayari wamekwishalipwa na kuondoka kupisha mradi.

Kwa mantiki hiyo aliwaelekeza TANESCO kushirikiana na Idara na Taasisi husika ili kushughulikia na kumaliza changamoto hizo zinazokwamisha malipo ya wananchi hao, na kuhakikisha wanawalipa wote kabla ya mwezi machi mwaka huu, ambapo kunatarajiwa kuwekwa jiwe la msingi la kuanza ujenzi wa mradi huo.

Sambasamba na hilo, alitaka kuhamishwa kwa makaburi yaliyopo katika eneo hilo kwa kufuata utaratibu na sheria za nchi, kuzingatia haki ya kila alieyepisha mradi huo, kuepuka malalamiko kutoka kwa wananchi.

“TANESCO kamilisheni ulipaji wa fidia kwa waliobaki, hizi changamoto zao zinatatulika shirikianeni na mamlaka husika pitieni nyaraka na kufuata sheria zinazotakiwa muwalipe fedha zao hawa wananchi, ili waendelee na maisha yao na mradi uanze kujengwa hapa, hatutaki mradi huu ulete malalamiko kwa wananchi tunataka haki itendeke kwa kila aliyepisha mradi huu na afurahie uwepo wake hapa, mapema mwezi Machi tutaweka jiwe la msingi, sitaki kusikia malalamiko siku hiyo,” alisema Wakili Byabato.

Aidha katika ziara hiyo, Wakili Byabato alitoa msisitizo kwa TANESCO, kuendelea kukata umeme kwa wadaiwa sugu ambao bado hawajalipa madeni ya Ankara zao na bado wanaendelea kutumia umeme.

Alisema ukataji wa umeme unawahusu wadaiwa wote bila kujali Taasisi, Mashirika ya Umma, Binafsi wala Dini.

Hata hivyo aliwasisitiza TANESCO kukata umeme kwa kuzingatia faida kwa maana kuwa mteja akilipa fedha kidogo atarejeshewa umeme kwa siku kadhaa, baadaye wakate tena hivyohivyo hadi pale atakapomaliza deni lake.

Vilevile wasikatae kupokea fedha ya mteja atakayoona anaweza kulipa kwa kipindi husika, wapokee wamuwashie baada siku kadhaa wakate tena.

Pia wawe na tabia ya kuwatembelea wadaiwa wao ili kuwakumbusha juu ya ulipaji wa madeni yao na kufanya ukaguzi ili kujiridhisha kama mteja aliyekatiwa umeme kwa muda mrefu  anatumia nishati gani, hiyo itasaidia kubaini wateja wasiowaaminifu wanaoiba umeme.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles