Na Renatha Kipaka
ZAIDI ya lita milioni 97.8 za maziwa zilikusanywa kwa matumizi mbalimbali kutoka kwa wafugaji wa ng’ombe wa maziwa kwenye wilaya nane za Mkoa wa Kagera kwa kipindi cha mwaka 2016/017 ikilinganisha na lita milioni 46.6 mwaka 2015/016
Makusanyo hayo yanatokana na taratibu zilizopo katika mkoa huo kujua zao hilo linanufaishaje jamii.
Ofisa Mifugo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, Colman John alisema lengo ni kila kaya kutumia maziwa na wafugaji kujipatia kipato.
Alikuwa akizungumza na wandishi wa habari ikiwa ni maandalizi ya maadhimisho ya wiki ya maziwa kuanzia Juni mosi mwaka huu.
John alisema tofauti hiyo ya ukusanyaj inatokana na mabadiliko ya tabianchi ambako ukame ulitawala na kusababisha kutokuwapo maji na nyasi za kutosha.
“Mabadiliko yanayotokea na kuonekana hapa ni ukame uliosababishwa na ukosefu wa mvua kwa muda mrefu na kusababisha ng’ombe kukosa lishe na maji,”alisema.
Alisema mkoa huo una ng’ombe wa maziwa wapatao 21,438 na ng’ombe wa asili 52,8632.
”Niseme tu kwamba taarifa hizo tunazipata kuanzia ngazi ya kijiji hadi wilaya maana wao ndiyo wanaojua ni nani anafuga na nani anayekamua maziwa kiasi gani,” alisema.
Meneja wa Kiwanda cha Maziwa Kagera katika o Manispaa ya Bukoba, Samwel John alisema kwa sasa upatikakanaji wa maziwa kwenye kiwanda hicho ni wa kiwango cha chini ikizingatiwa hukusanya lita 200-300 za maziwa kwa siku ndani ya manispaa hiyo.
Alisema awali kiwanda hicho kilikuwa kinapata maziwa kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya lakini kwa sasa hayapatikani kwa wingi.
“Kama sisi hapa tunazalisha maziwa aina tatu, maziwa fresh, yogati na mtindi kwa uwiano wa lita 150 ni fresh, lita 100 ni yogati na lita 50 matumizi ya watu majumbani,” alisema John.
Naye Methodi Karikira, mtumiaji wa maziwa klra siku na mkazi wa Manispaa ya Bukoba, alisema ulipotokea ukame maziwa yalikuwa ya shida kupatikana hata katika familia.
Alisema sababu nyingine ya upungufu wa maziwa ni ardhi kutokuwa na madini ya chumvi na kufanya wafugaji kuwapa ng’ombe wao chumvi ya kawaida kwa wingi.