25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Bugando kufanya utafiti ugonjwa wa figo, moyo

Clara Matimo -Mwanza

HOSPITALI ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa Bugando (BMC), imepanga kutumia Sh milioni 60 kufanya utafiti ili kubaini vyanzo na viashiria vya magonjwa sita yasiyo ya kuambukiza katika mikoa sita na wilaya 12 zilizopo Kanda ya Ziwa.

Utafiti huo utafanywa na hospitali hiyo kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Kanisa  Katoliki cha Sayansi ya Afya na Tiba Bugando (CUHAS) vya jijini Mwanza.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini hapa, Mkurugenzi wa BMC, Profesa Abel Makubi, aliyataja magonjwa hayo kuwa ni moyo, mgandamizo wa moyo, figo, saratani, kisukari na uzito kupita kiasi.

 Alisema wameamua kufanya utafiti huo ili kupata takwimu zinazotosheleza kwa sababu walizonazo hazitoshelezi kubaini vyanzo na viashiria.

Profesa Makubi alisema ingawa wanatoa huduma ya magonjwa hayo hospitalini hapo, lakini wanaamini wapo wagonjwa wengi vijijini ambao hawafiki hospitalini.

“Huu ni utafiti wa awali, tutawafikia wananchi 770, tutawafuata vijijini kabisa, lengo ni kutaka kujua viashiria vinavyoweza kuhusika na magonjwa hayo, uelewa wa watu kuhusu magonjwa hayo, pia uwezo wa vituo vya afya kwenye maeneo hayo kugundua magonjwa hayo.

“Hapa BMC kwa wiki wagonjwa wanaosafishwa figo wanazidi 100, wagonjwa wa kiharusi wawili, kisukari tunaona wagonjwa wapya watano kila siku, presha kila siku tunaona  wagonjwa watano na kliniki kwa wiki wanaonwa wagonjwa 70,  asilimia 25 hadi 30 ya wagonjwa tuliowalaza wodini wana ugonjwa huo,” alisema.

Mhadhiri Mwandamizi wa CUHAS, Dk. Anthony Kapesa, alisema utafiti huo utahusisha madaktari bingwa 12 na watafiti wasaidizi zaidi ya 200.

“Utafiti huo utafanyika Mkoa wa Mwanza katika Wilaya ya Sengerema na Misungwi, Shinyanga tutafanya Wilaya ya  Kishapu, Geita tutakuwa vijijini na Wilaya ya Chato, Mkoa wa Kagera tutafanya wilaya ya Muleba na Bukoba Vijijini, Simiyu tutafanyia Wilaya ya Bariadi na Busega na Mkoa wa  Mara tutaenda Wilaya ya Serengeti na Bunda,” alisema

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles