Na Esther Mnyika,Mtwara
BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imewataka wananchi kutotunza noti au sarafu ndani badala yake waziingize katika mzunguko au kuweka katika taasisi za fedha ili ziendelee kuwa katika uzalishaji.
Hayo ameyabainisha leo Februari, 26 2025 mkoani Mtwara na Afisa wa BoT kutoka Kurugenzi ya Usimamizi wa Sarafu, Itika Mwakisambwe wakati akiwasilisha mada ya historia ya fedha ya Tanzania, alama za usalama na utunzaji fedha katika mafunzo ya Waandishi wa habari za uchumi kutoka mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Dar es Salaam na Visiwani Zanzibar.

“Utunzaji mzuri wa shilingi ya Tanzania utawezesha kuakaa katika mzunguko wa shughuli za uchumi kwa muda mrefu na gharama ambazo zingetumika kutengeneza fedha mpya kuelekezwa kwenye miradi ya Maendeleo,” amesema Itika.
Amesema BoT imekuwa ikitumia gharama kubwa ya fedha za kigeni na kutengeneza fedha zinazotumika nchini hivyo inawajibu kuhakikisha kuna fedha safi katika mzunguko mda wote na uharibifu wowote ule wa fedha haukubaliki nchini.
Akizungumzia kuhusu ukunjaji wa fedha za noti Itika amesema wale wote wenye tabia ya kuunganisha noti kwa kutumia pini au stempu hivyo wanapaswa kuacha mara moja kufanya hivyo ni uharibifu wa fedha na kuchakaa haraka.

Amesema kila mmoja anapaswa kutunza, kuacha au kupunguza kuzikunja fedha za noti hivyo kukunja kuputa kiasi kunadhoofisha karatasi na inaweza kukatika.
“Fedha zishikwe tukiwa na mikono safi mikavu asilimia 100 ya noti zetu zinatengenezwa kwa pamba ukishika na mikono michafu zinachafuka na kuharibika pia tunapaswa kuithamini na kuitunza vizuri fedha yetu ili iweze kudumu katika mzunguko,” amesema.