NORA DAMIAN Na ASHA BANI-DAR ES SALAAM
BOMOABOMOA nyingine inatarajia kuwakumba wakazi wa Mkoa wa Dar es Salaam kupisha upanuzi wa Barabara ya Morogoro.
Tayari Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) Mkoa wa Dar es Salaam, ameanza kuweka alama za X katika baadhi ya nyumba zilizo pembezoni mwa barabara hiyo ambazo zinatakiwa kubomolewa kupisha ujenzi huo.
MTANZANIA jana lilitembelea maeneo mbalimbali ya barabara hiyo na kushuhudia nyumba kadhaa na maduka ya biashara yaliyo pembezoni mwa barabara hiyo kuanzia eneo la Kimara Mwisho hadi Kimara Temboni zikiwa zimewekwa alama ya X.
Mbali ya nyumba za watu binafsi pia kituo cha mafuta cha Total kilichoko Kimara Temboni na Hospitali ya Neema vitabomolewa.
Meneja wa Tanroads Mkoa wa Dar es Salaam, Julius Ndyamukama, alisema wanatarajia kuanza mradi wa upanuzi wa barabara hiyo kuanzia eneo la Kimara Mwisho hadi Kiluvya.
Alisema hifadhi ya barabara ya Morogoro ina upana wa mita 121.5 kutoka katikati mwa barabara kila upande.
Alisema wakazi hao wanatakiwa kubomoa nyumba hizo ndani ya siku 30 kuanzia siku walipopewa notisi na kwamba watakaokaidi nyumba zao zitabomolewa na watalazimika kulipa gharama zote zitakazojitokeza katika utekelezaji wa hatua hiyo.
Hata hivyo baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili walilalamikia kutoshirikishwa katika mchakato huo na kudai kuwa wameshtuka wakipewa notisi.