30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Beki Simba afichua siri yake, Wawa

 WINFRIDA MTOI, – DAR ES SALAAM 

BEKI wa kati wa Simba, Kennedy Juma, amefichua siri ya ubora wake anapopewa nafasi ya kucheza, akisema ni kutokana na maelewano yake mazuri na Pascal Wawa. 

Juma alisajiliwa na Wekundu wa Msimbazi hao, msimu huu akitokea Singida United. 

Akizungumza jana katika kipindi maalum cha maswali na majibu kutoka kwa mashabiki kupitia mitandao ya Simba, mchezaji huyo, alisema tangu ametua kikosini hapo, amekuwa akicheza na Wawa. 

Alisema mara nyingi akicheza na beki huyo raia wa Ivory Coast, anakuwa bora kwa sababu anamwelekeza vizuri vitu vya kufanya ili kulinda ngome yao. 

“Mara nyingi napangwa kucheza na Wawa, nimeona ni beki tunayeelewana na kutengeneza pacha nzuri, ananituma na mimi nafuata kila anachonieleza na kunifanya niwe huru na makini,” alisema. 

Ataja beki anayemkubali Tanzania 

Juma alisema kati ya mabeki wote nchini, anamkubali zaidi Erasto Nyoni tangu akiwa hajatua Msimbazi. 

“Nyoni ni beki ninayemkubali kwa muda mrefu” 

Aikumbuka Yanga 

Alisema mechi anayoikumbuka zaidi ni ile ya mzunguko wa pili waliyokutana na Yanga na kufungwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam. 

Alisema katika mchezo huo, aliingia kipindi cha pili baada Nyoni kuumia, lakini kabla ya kuingia uwanjani ilibidi asimame kuomba Mungu ili akafanye kile alichoelekezwa. 

“Mechi inayoikumbuka ni ile tuliyocheza na Yanga, mwalimu alinipa maelekezo ya kwenda kufanya, ilibidi nimuombe Mungu kwanza, nashukuru nilifanikiwa kutekeleza yale niliyoambiwa,” alisema. 

 Pia, aliitaja mechi dhidi ya Polisi Tanza

 nia kuwa iliwatoa jasho kutokana na wapinzani wao kuonesha ubora wa hali ya juu.

“Mechi na Polisi Tanzania ilikuwa ngumu sana kwetu, nafikiria sana ilikuwaje kwa sababu kazi tulifanya ni kubwa hadi kupata ushindi,” alisema.

Changamoto alizopitia hadi kutua Simba

Alieleza kuwa haikuwa safari rahisi hadi kutua Msimbazi kulingana na timu alizopitia, akianzia Singida United tangu ikiwa Ligi Daraja la Pili.

“Nimepita katika changamoto nyingi, lakini sikukata tamaa, hadi nikafikia kusajiliwa na timu kubwa kama Simba, anaendelea kujifunza mambo mengi,” alisema.

Alieleza maisha ya sasa ndani ya Simba, kuwa ni mazuri tofauti na timu nyingine ikiwamo kupata mshahara kwa wakati na uongozi kuwa wepesi kutatua matatizo cha wachezaji.

“Maisha ya Simba ni raha, unapata kila unachotaka na mshahara kwa wakati, changamoto zipo kila sehemu, muhimu kujipanga kukabiliana nazo,” alisema Juma.

Alisema Simba kuna ushirikiano mkubwa wa wachezaji na ndiyo sababu ya kufanya vizuri katika mechi zao.

Ndoto zake

Alifafanua kuwa pamoja na kucheza Simba, ana ndoto za kucheza soka la kulipwa nje ya nchi, lakini pia akistaafu atajikita katika kilimo na ufungaji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles