23.3 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Bavicha: Polisi wasingeweza kutuzuia

Patrobas Katambi
Patrobas Katambi

NA AZIZA MASOUD, DAR ES SALAAM

BARAZA la Vijana la Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha), limetoa kauli yenye mwelekeo wa kupimana ubavu na Jeshi la Polisi, kuhusu msaada lililokusudia kuutoa, kuzuia kufanyika kwa mkutano mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Dodoma.

Kwamba kusudio la jeshi hiloMkuwazuia kwenda Dodoma, lisingefanikiwa kwa madai kuwa
Bavicha ina nguvu kuliko polisi.

Kauli hiyo, imetolewa jana Ofisi za Makao Makuu ya Chadema na Mwenyekiti wa Bavicha, Patrobas Katambi, katika mkutano wake na waandishi wa habari kuhusu msimamo wa baraza hilo kuelekea Mkutano Mkuu wa CCM uliopangwa kufanyika Julai 23.

Katambi alisema Bavicha imeamuakutokwenda Dodoma kwa sababu ya kutii kauli ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, huku akisisitiza kuwa Mkutano Mkuu wa CCM utakaofanyika wiki ijayo si halali, hivyo Serikali inapaswa kutoa kauli itakayoonyesha kuwapo kwa haki sawa za kidemokrasia kwa kila chama.

Alisema Bavicha lilipanga kuzuia Mkutano Mkuu wa CCM kwa sababu si halali kwa kuzingatia kauli zilizotolewa na baadhi ya viongozi wa Jeshi la Polisi pamoja na Rais John Magufuli, kwamba wanasiasa wanapaswa kusitisha shughuli za kisiasa hadi mwaka 2020.

“Tulikuwa tumeshajipanga, CCM wasingeweza kutuzuia, hata polisi wenyewe wasingekuwa na
ubavu wa kutuzuia. Washukuru kauli ya Mwenyekiti wa Taifa, Freeman Mbowe imeleta unafuu kwa sababu kiutaratibu akiongea yeye kama kiongozi, ni maagizo lazima yafuatwe.

“Idadi ya polisi na silaha isingeweza kutuzuia kwa sababu tulikuwa hatuendi kupambana na polisi, bali kupagania demokrasia kwa njia ya halali. Lengo la kwenda Dodoma haikuwa kufanya vurugu, bali kupata usawa wa demokrasia na kuondoa upendeleo,” alisema.

Katambi alieleza zaidi kuwa Bavicha haitakubali nchi iongozwe kwa upendeleo, kwa kauli za viongozi ambazo hazifuati sheria na katiba ya nchi, na kwamba Watanzania waone na wapaze sauti kuhusu namna nchi yao inavyoongozwa kidikteta kwa kukosa usawa.

Alieleza kushangazwa na hatua ya polisi kutoka mikoa ya Morogoro, Singida, Dar es Salaam naIringa kupelekwa Dodoma wakiwa na vifaa vya kivita kwa ajili ya kulinda mkutano wa kisiasa jambo aliloeleza kuwa halijawahi kutokea.

“Hatutaenda Dodoma, lakini tumeamua kuja na ‘plan’ (mpango) B, hatutaruhusu mkutano wa CCM ufanyike mpaka Serikali itakapotoa kauli ya haki sawa ya demokrasia kwa kila chama katika kufanya siasa. Hivi tunavyoongea CCM wao wanafanya mikutano ya hadhara wakati wengine wanazuiwa,” alisema Katambi.

Mwenyekiti huyo wa Bavicha, alionya kuwa iwapo Rais Magufuli
atahudhuria mkutano huo, atakuwa amekwenda kinyume na maagizo yake jambo ambalo ni hatari. Pia alimtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu kujiuzulu iwapo mkutano huo utafanyika.

Wakati huo huo, Katambi jana alitangaza kuwa Kamati Tendaji ya Bavicha inatarajiwa kukutana Julai 20, huko Dodoma katika kikao ambacho pia kitahudhuriwa na Mbowe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles