30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Bangili ya mkia wa tembo yampeleka jela

mkia wa tembo

NA MANENO SELANYIKA,

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemhukumu jela kifungo cha miaka mitano au kulipa faini ya Sh milioni 65.8 raia wa Afrika Kusini, Rudolf Van Niekerk (68), kwa kosa la kutaka kusafirisha bangili moja iliyotengenezwa kwa manyoya ya mkia wa tembo.

Akisoma hukumu hiyo jana Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Huruma Shahidi, alisema amesikiliza hoja za utetezi pamoja na zile za upande wa Jamhuri hivyo kumtaka mtuhumiwa kutumikia adhabu hiyo endapo atashindwa kulipa kiasi hicho cha fedha.

“Mtuhumiwa utatumikia jela miaka mitano au ulipe fedha hizo kwa kuwa sheria za nchi hii zinakataza kusafirisha nyara za Serikali bila kuwa na kibali,” alisema Hakimu.

Awali wakili wa upande wa Jamhuri, Paul Kudushi, akisoma hati ya mashtaka ya mtuhumiwa huyo alidai tukio hilo lilitokea Juni 17 mwaka huu ambapo mtuhumiwa akiwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl JK Nyerere (JNIA), alikamatwa akitaka kusafirisha bangili hiyo ambayo thamani yake ni Dola za Marekani milioni 15 sawa na shilingi za Kitanzania  zaidi ya milioni 32.

Aidha, Wakili aliiomba mahakama impe adhabu kali mtuhumiwa huyo kwa kuwa ameisababishia hasara Serikali kwa kusafirisha nyara bila kibali lakini pia ameteketeza viumbe ambavyo ni tunu kwa Taifa letu.

“Mheshimiwa kwa kuwa mtuhumiwa amekiri kufanya kosa hilo, hivyo tunaomba mahakama hii tukufu impe adhabu kali kwani vitendo vya kusafirisha nyara za Serikali vimekithiri hasa kwa raia wa kigeni,” alidai Wakili wa Jamhuri.

Kwa upande wa utetezi ambapo mshtakiwa alikuwa anawakilishwa na Wakili Gerald Nangi, aliomba mahakama hiyo impunguzie adhabu mteja wake kwa kuwa si raia wa Tanzania na kwamba kuna baadhi ya sheria alikuwa hajui ikiwemo hiyo.

Nangi pia alidai kuwa mteja wake anasumbuliwa na maradhi mbalimbali na anatumia dozi kwa ajili ya maradhi yanayomsumbua.

Zaidi Wakili aliiomba mahakama hiyo impunguzie adhabu kwani ni mara ya kwanza kwa mteja wake kupatikana na kosa tangu alipokuja hapa nchini.

“Mheshimiwa licha ya hiyo mteja wangu ni mtaalamu mzuri wa masuala ya uhandisi wa umeme na wakati alipokuwa hapa nchini alikuwa anafanya kazi katika kiwanda cha sukari kilichopo Kilombero mkoani Morogoro.

“Amekuwa mstari wa mbele kupigania upatikanaji wa sukari kwa wingi hasa kipindi kulipokuwa na uhaba na kwamba mteja wangu ana mke na watoto wanaomtegemea kama baba wa familia,” alidai wakili wa utetezi.

Akizungumza nje ya Mahakama na gazeti hili, Nangi alisema walikuwa wanafanya mchakato kuhakikisha mteja wake analipa faini hiyo na si kwenda jela.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles