Jessca Nangawe -Dar es salaam
BEKI wa zamani wa Simba, Abdi Banda amesaini mkataba wa miaka miwili wa kuitumikia Highlands Park inayoshiriki Ligi Kuu nchini Afrika Kusini.
Banda ambaye kabla ya kutua ndani ya klabu hiyo alikua akiikipiga Baroka FC, sasa atakua akiingiza mkwanja mrefu zaidi.
Kwa mujibu wa mtu aliye karibu ni beki huyo, atakua anaweka kibindoni kitita cha randi 150,000(zaidi ya Sh milioni 24 za Kitanzania).
Banda aliachana na Klabu ya Baroka FC, baada ya kumaliza mkataba wake na kutoafikiana kuongeza mwingine na waajiri wake hao wa zamani.
Majeraha yaliyomwandama msimu uliopita yanadaiwa kuwa sababu ya Baroka kutoshawishika kuendelea kumpa maisha beki huyo.
Kabla ya kutua Baroka, Banda alikuwa akiichezea Simba ambayo ilimsajili kutoka Coastal union ya Tanga.