Na Mwandishi Wetu
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO),limetoa taarifa ya uwepo wa maboresho katika kituo cha kupokea, kupoza na kusambaza umeme cha Msongo wa Kilovoti 220 cha Ubungo kilichopo jijini Dar es Salaam kuanzia February 22- 28, 2025, hivyo baadhi ya maeneo ya Zanzibar na mikoa ya Dar es Salaam na Pwani yataathirika kwa kukosa umeme kwa nyakati tofauti.
Katika taarifa ya TANESCO iliyotolewa leo February 19,2025 imesema hatua hiyo ni muhimu kwa Shirika kuboresha utoaji wa huduma kwa wateja wake kufuatia ongezeko la mahitaji ya matumizi ya umeme katika maeneo ya Zanzibar, Dar es Salaam na Pwani ambalo limefanya kituo hicho kuzidiwa na hivyo kulazimu kufungwa kwa mashine mpya (Transformer) kubwa yenye uwezo wa MVA 300 ili kukidhi mahitaji ya umeme katika maeneo tajwa.
“Katika kipindi hicho ambacho huduma ya umeme itakosekana kwa nyakati tofauti Shirika pia litakuwa likifanya matengenezo mbalimbali ya miundombinu ya umeme kwenye maeneo tajwa ili kuiweka miundombinu yetu kenye hali ya imara hasa kwenye kipindi hiki tunachoelekea cha msimu
wa mvua.
“Shirika linaomba radhi kwa usumbufu katika kipindi chote ambacho huduma ya umeme itakosekana kwenye baadhi ya maeneo na litaendelea kutoa taarifa za maendeleo ya kazi hiyo mpaka kukamilika kwake,” imesema taarifa hiyo.
