28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

ATI yaleta maombi kuongeza uwekezaji nchini

MWANDISHI WETU-DODOMA

KAMA ilivyo kwa nchi nyingine za Afrika, Tanzania inawekeza katika uboreshaji wa miundombinu yake ili kukuza utalii na kuvutia wawekezaji.

Katika mazungumzo kati yake na Serikali ya Tanzania, Shirika la Bima la Afrika (the African Trade Insurance Agency – ATI) imetoa mapendekezo yatakayoisaidia nchi kuvutia wawekezaji.

Mapendekezo ya ATI pia yananuia kuisaidia nchi kupunguza gharama za kukopa kwa miradi ya baadaye kwa kati ya Dola za Marekani milioni mbili hadi tatu kwa mwaka kwa muda wa miaka kumi au zaidi. 

Tanzania ni mwanachama mwanzilishi wa ATI – taasisi ya kimataifa na ya kiafrika inayojishughulisha na kutoa dhamana za uwekezaji na mikopo ili kusadia nchi wanachama kukuza viwango vya wawekezaji.

Katika mfumo unaopendekezwa, ATI itatoa aina ya dhamana ya mikopo ijulikanayo kama ‘credit wrap’ kwa lengo la kusaidia nchi kupata unafuu wa riba inapopeleka maombi ya mikopo katika soko la kimataifa.

Katika mfumo unaopendezwa (wa credit wrap), tayari ATI imeshazisaidia nchi kadhaa za Afrika kupata mikopo kwa riba nafuu ambapo mwaka 2019, nchi za Benin na Cote d’Ivoire zilibahatika kupata mikopo inayofikia karibu Dola za Marekani bilioni 1 (zaidi ya Sh trilioni 2.3).

Mikopo hiyo itakuwa na riba za kiwango cha chini cha digiti moja (chini ya asilimia 10) na kulipwa kwa miaka zaidi ya 10 hadi 12.

Kwa muda mrefu, imekuwa ngumu sana kwa nchi za Afrika kupatiwa masharti nafuu kama haya ya mikopo.

Hii imetokana na ukweli kuwa ukanda wa Afrika huchukuliwa kuwa na hatari kubwa ya mikopo kutokurudishwa kwa wakati na hivyo kwa muda mrefu ukanda huu umekuwa na upungufu wa bima ya mikopo.

“Lengo la ATI ni kuziba pengo hili la bima ya mikopo kwa kutoa dhamana zinazohitajika kwa nchi wanachama wake,”  alisema Mkurugenzi wa Kampuni ya Wakala wa Bima Tanzania, Tusekile Kibonde, wakati wa mkutano na wadau wa maendeleo ya bima kubwa nchini uliofanyika Wizara ya Fedha na Mipango na kuratibiwa na taasisi ya Africa Trade Insurance (ATI) uliofanyika jijini Dodoma jana.

Uwezo wa ATI kufanya kazi hiyo umepewa shime na uaminifu wake unaotokana na kupewa alama za juu za upimaji wa viwango vya uwekezaji uliofanywa na Kampuni ya S&P and Moody’s.

S&P and Moody’s ni kampuni ya kimataifa ya utafiti na upimaji wa utoshelevu wa nchi au tasisisi katika kupata mikopo ya kimataifa.

Kwa miaka mitano iliyopita, ATI imeisaidia Tanzania katika maeneo kadhaa ya uwekezaji.

Maeneo hayo ni pamoja na katika mradi wa Sh trilioni 2 wa ujenzi wa reli ya kisasa.

ATI pia imesaidia katika maeneo mengine ya kuvutia uwekezaji katika sekta za fedha, nishati na miundombinu.

Ikiwa na uwekezaji wa Dola za Marekani milioni 447 (ambazo ni zaidi ya Sh trilioni moja) hapa nchini, ATI inaamini kuwa ipo katika nafasi nzuri ya kuisaidia Tanzania kuongeza zaidi uwekezaji.

Mkuu wa Idara ya Huduma za Kifedha wa Benki ya NMB, Linda Teggisa alisema; “Tukiwa kama benki inayoongoza kwa faida Tanzania, tupo pamoja na Serikali kuchangia maendeleo endelevu kwa kubuni mifumo ya kisasa na kwa kushirikiana na wadau kama ATI ili kufikia malengo ya 2025 ya kiuchumi, hususan kwenye miundombinu.”

Naye Kaimu mkurugenzi wa wateja wakubwa wa Benki ya CRDB, Prosper Nambaya alisema ushirikiano baina ya benki yake na ATI umefanikisha ufadhili wa miradi mingi mikubwa ya ujenzi wa miundombinu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles