27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Askofu wa Katoliki aeleza njia mpya kuzuia Katiba

Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Askofu Severin Niwemugizi
Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Askofu Severin Niwemugizi

NA NORA DAMIAN, DAR ES SALAAM

MAKAMU wa Rais Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Askofu Severin Niwemugizi, amesema maoni yaliyotolewa na Jukwaa la Wakristo Tanzania (TCF) juu ya Bunge Maalumu la Katiba, hayajatekelezwa na hivyo watapita kwa Watanzania na waumini wao kuwaeleza nini cha kufanya.

Jukwaa hilo lilikutana Agosti 27 hadi 28, mwaka huu na kujadili hatima ya Bunge hilo na kutoa mapendekezo sita, moja ikiwa ni kusitishwa kwake.

Akizungumza na gazeti hili jana, Niwemugizi  ambaye pia ni mjumbe wa TCF, alisema: “Tunaona Bunge bado linaendelea na Serikali iliyopo madarakani inaendelea na mipango yake, haiheshimu wala haitekelezi ushauri unaotolewa.

“Sauti nyingi haziridhiki na yale yanayotendwa na Bunge Maalumu la Katiba, hawajui ni kiasi gani Watanzania wameshapevuka na wanatambua haki zao.”

Alisema wamejipanga kurudi kwa Watanzania kuwafahamisha na kuwafundisha ili watambue haki na wajibu wao hali itakayowasaidia kujua njia sahihi ya kufanya.

“Wanaweza kutudharau kwamba sisi hatuna chochote, kwakuwa hawajali tuliyopendekeza, tutarudi kwa watu wetu tunaowaongoza, kitakachotokea hatujui.

“Sisi tunaamini kurudi kwa Watanzania ni sehemu pia ya injili kwa sababu kuna injili ya jamii, na tutawafundisha watambue haki na wajibu wao na namna sahihi ya kufanya,” alisema.

Askofu huyo alisema wanachotaka Watanzania ni kuona mambo yakienda vizuri, hivyo kama viongozi wanakataa ushauri unaotolewa, Watanzania wataamua cha kufanya.

Kuhusu Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, askofu huyo alisema amejidhalilisha kwa kauli zake za kejeli ndani ya Bunge hilo.

“Mkishakuwa na viongozi wenye dharau na kejeli, hapo nchi imekwisha kabisa. Sitta amejidhalilisha kwa kauli zake, hasa ukizingatia kuwa na yeye anatajwa kutaka kugombea urais, sifa zake zinazidi kupungua,” alisema.

Jukwaa hilo linaundwa na Baraza la Maaskofu Katoliki (TEC), Baraza la Makanisa ya Kipentekoste (CPCT), Jumuiya ya Kikristo (CCT) na Makanisa ya Kisabato (SDA).

Tamko la jukwaa hilo lililotolewa Agosti 28, mwaka huu, lilisema mjadala wa Bunge hilo umeondoa maoni yaliyotolewa na wananchi kuhusu muundo wa Muungano, kupunguza mamlaka ya Rais, uwajibikaji na uwajibishwaji wa wabunge na ukomo wao.

“Wamewezesha maoni na maslahi ya chama tawala kwa uongozi wa kikundi cha wanasiasa wachache wasio na uaminifu na uadilifu wa kutosha kuwekwa kama mapendekezo ya Katiba mpya kwa nia ya kulinda maslahi binafsi au ya makundi na kuhalalisha ukiukwaji mkubwa wa sheria, kanuni na maadili ya uongozi bora,” inasema sehemu ya tamko hilo.

Kutokana na hali hiyo, jukwaa hilo lilitoa mapendekezo sita likitaka yafanyiwe kazi.

MAPENDEKEZO YA JUKWAA

1. Serikali (Wizara ya Katiba na Sheria) irudishe tovuti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na nyaraka zake zote kwa ajili ya wananchi kuendelea kuona kazi waliyoifanya, kujifunza na kujadili Rasimu ya Katiba kwa uwazi.

2. Bunge Maalumu la Katiba linaloendelea lijadili na kuboresha tu maoni yaliyomo katika Rasimu ya Katiba na sio kufanya mabadiliko katika Katiba ya mwaka 1977.

3. Mchakato wa Katiba usimamishwe ili kupisha majadiliano, maelewano na maridhiano mwafaka, Uchaguzi Mkuu na wa Serikali za Mitaa. Na mabadiliko ya Katiba ya 15 ya mwaka 1977 yafanyike kuwezesha chaguzi kufanyika kwa uwazi na haki. Pia, kuweka kifungu kitakacholinda rasimu ya pili na kumtaka kiongozi ajaye kuendelea na mchakato wa Katiba.

4. Baada ya Bunge Maalumu la Katiba kuanza shughuli zake tena, Mwenyekiti wa Bunge hilo afanye kazi kwa mujibu wa kanuni na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba badala ya kutumia ubabe na kiburi cha wingi wa wajumbe wa Chama cha Mapinduzi katika Bunge la Katiba.

5. Wananchi waendelee kusoma na kujadili maoni yaliyoko katika rasimu ya pili ya Katiba, na kufuatilia kitakachokuwa kinajadiliwa kwenye Bunge la Katiba ili kuwawezesha kupiga kura ya maoni wakiwa na uelewa wa kutosha kabisa kuhusu ni nini kipo kwenye “Katiba inayopendekezwa”. Wananchi pia wajitokeze kwa wingi kujiandikisha kwa nia ya kuwawezesha kupiga kura ya maoni.

6. Tume ya Mabadiliko ya Katiba ihuishwe na kupewa mamlaka kisheria ili kuiwezesha kujibu maswali yanayojitokeza na kutoa ufafanuzi kwa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi kwa jumla hadi Katiba mpya itakapokamilika na kukabidhiwa rasmi.

Tamko lilisema: “Jukwaa la Wakristo Tanzania na Watanzania wote wanaoitakia nchi yao mema, tunakuomba Mheshimiwa Rais kwamba AMANI ya nchi yetu sasa imo mikononi mwako, hasa katika kipindi hiki cha kuandikwa kwa Katiba mpya.

“Tunakuomba uahirishe mchakato unaoendelea ili uepushe ishara za aina mbalimbali za kuanzisha sintofahamu nchini mwetu na hali yoyote inayoweza kuathiri vibaya mshikamano, umoja na amani ya taifa letu.

“Ifahamike kuwa Wananchi wa Tanzania wako juu ya Wajumbe wa Chama cha Mapinduzi. Kwa mantiki hiyo, tunakuomba uepushe wananchi wa Tanzania kuhamasishwa kukikataa Chama cha Mapinduzi kwa kuwa tu chama hicho kimeyapuuza na kimekataa maoni yao waliyotoa kwa dhati baada ya kuaswa na kuhimizwa kufanya hivyo na viongozi wa nchi.

“Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wafanye yasiyowapasa.

“Wamejawa na udhalimu wa kila namna, uovu na uuaji, na fitina, na hadaa; watu wa nia mbaya, wenye kusengenya, wenye kusingizia, wenye kumchukia Mungu, wenye jeuri, wenye kutabakari, wenye majivuno, wenye kutunga mabaya, wasiowatii wazazi wao, wasio na ufahamu, wenye kuvunja maagano, wasiopenda jamaa zao, wasio na rehema; si hivyo tu, bali wanakubaliana nao wayatendao. (Rejea Warumi 1: 28-32)

“Ikumbukwe kuwa Rasimu ya Pili ya Katiba ni waraka halali na rasmi na ndiyo mawazo ya Watanzania na tunahimiza kuwa Katiba ni ya wananchi na inahitaji maridhiano na siyo ubabe.”

- Advertisement -

Related Articles

17 COMMENTS

  1. Haya sasa kazi kwa CCM na serikali yake pamoja na Rais na Spika wa Bunge la katiba. Tukisema ukweli kwamba CCM mnamdharau hata kwa viongozi wa dini mnasema akina Mapunda wanachochea chuki na kutukana vibaya. Sasa leo yapowapi? Viongozi wa kanisa hongereni rudinikwa wananchi mimi nitakuwa mmoja wapo wa kuzunguka Tanzania nzima kuhubiri ukweli huo sihitaji hata senti tano ya mtu. Injili ya jamii ipo na ndiyo wengine tunahubiri watu kujua haki zao, siyo kila wakati kusingizia kulinda amani na kutumia kigezo hicho kwa polisi kujeruhi na kuua raia hovyo. Amani gani inalindwa kwa bunduki, CCM imekufa na tunasubiri hurufu yake tu basi. Hongera Askofu Severinus nafahamu msimamao wako, hongere Askofu wa KKKT Sumbawanga kwa kumtolea uvivu waziri mkuu. Kiburi cha CCM ni mauti yenu mjue hilo, hamwezi kudharau watu milioni 45, nyie nani? Mungu wabariki viongozi wa Jukwaa la Wakristo na uwalinde daima. Hii ni habari njema ya ukombozi wa pili wa Watanzania kutoka kwa wakoloni weusi -CCM.

    • Hongereeni Maaskofu. katika siku ambazo nimefurahia ni hii. unajua Rais Kikwete anafikiri kuwa atasalimika na uharibifu unaofanywa na Sitta kwa kumwangalia tu na asiseme chochote. na wasijifariji kuwa kwa kitendo wanachokifanya wakiwa kwenye viti vyekundu cha kutuburuza ili wafanye matakwa yao wakifikiri watatawala milele hatukioni. tunakuona na tunajua vyema nia yao. Gaddaffi naye alifikiri atatawala milele lkn ndo kila mtu anajua kifo cha aibu cha mkuu huyo cha kuuawa kama panya. list ya wabunge wanaoendelea kuwepo bungeni inajulikana na iko siku moja katika maisha yao watapaswa kuwajibika kwa hilo.

      maaskofu kazeni kamba maana mpaka hapa hatuna imani hata na Rais kikwete. mbwa uliyemfuga ataendelea kuwa mtii kama utamstahi ila ukimbana kwenye kiti ulichokikalia atatafuta njia ya kuondokana na maumivu akishindwa kabisa atakuuma. kwa hiyo CCM imetukalia kwenye kiti huku wakiendelea na kunywa Maji na soda nk na huku tukipata maumivu wao raha. wajue wazi kuwa meno yanaota na iko siku tutajitetea.

      wito Wangu kwa maaskofu wote washiriki toeni sauti zenu zisikike Lila mmoja kuonyesha umoja na mshikamano wetu. washirika tuko nyuma yenu.

      mbarikiwe na Bwana.

  2. Hongereeni Maaskofu. katika siku ambazo nimefurahia ni hii. unajua Rais Kikwete anafikiri kuwa atasalimika na uharibifu unaofanywa na Sitta kwa kumwangalia tu na asiseme chochote. na wasijifariji kuwa kwa kitendo wanachokifanya wakiwa kwenye viti vyekundu cha kutuburuza ili wafanye matakwa yao wakifikiri watatawala milele hatukioni. tunakuona na tunajua vyema nia yao. Gaddaffi naye alifikiri atatawala milele lkn ndo kila mtu anajua kifo cha aibu cha mkuu huyo cha kuuawa kama panya. list ya wabunge wanaoendelea kuwepo bungeni inajulikana na iko siku moja katika maisha yao watapaswa kuwajibika kwa hilo.

    maaskofu kazeni kamba maana mpaka hapa hatuna imani hata na Rais kikwete. mbwa uliyemfuga ataendelea kuwa mtii kama utamstahi ila ukimbana kwenye kiti ulichokikalia atatafuta njia ya kuondokana na maumivu akishindwa kabisa atakuuma. kwa hiyo CCM imetukalia kwenye kiti huku wakiendelea na kunywa Maji na soda nk na huku tukipata maumivu wao raha. wajue wazi kuwa meno yanaota na iko siku tutajitetea.

    wito Wangu kwa maaskofu wote washiriki toeni sauti zenu zisikike Lila mmoja kuonyesha umoja na mshikamano wetu. washirika tuko nyuma yenu.

    mbarikiwe na Bwana.

  3. Askofu hubiri dini na sio siasa.Vinginevyo vua joho hilo tuweze kukujuza vyema.Nchi haina dini na iliamuliwa hivyo kwa faida ya watu wote wa Tanzania.Hivi unawezaji kusema Rasimu ya katiba ya Warioba ni ya wananchi wakati kuna mapungufu makubwa mno kuanzia takwimu zilivyokusanywa hadi uandishi wake.Hata hivyo Rasimu hiyo sio mali ya Warioba na wenzake. Kuendeleo kushindikiza unayodai tunakuwa na mashaka na azma yako.

  4. Ndugu Ngowi unamuonya Askofu wako kwa kuwa tu amesema ukweli. Umempa andiko la kujisahihisha yeye kwanza. Angalia usiwe unapingana na maagizo ya Mungu. Hebu soma andiko hili: “Nimwambiapo mtu mbaya, Ewe mtu mbaya, hakika utakufa nawe husemi neno la kumwonya mtu huyo, aiache njia yake, mtu mbaya huyo atakufa katika uovu wake, lakini damu yake nitai (Ezekieli 33:8). Askofu asipokemea uovu unaoendelea katika utawala wa CCM iko siku atajibu mbele za Mungu. Je wewe utamtetea siku hiyo?

  5. SITTA NI JANGA LA KITAIFA
    HAKIKA MWENYEKITI WA BMK SAMWELI SITTA HAFAI HATA KUWA MJUMBE WA NYUMBA KUMI. ASHAKHUM MZEE HUYO NI MNAFIKI ANAYEPIGANIA MASLAHI YAKE TU WALA SI YA CCM. SHIDA YAKE NI URAISI. NA HAKIKA HATAUPATA HATA AKITUMIA HILA ZILIZOJE, MWENYEZI MUNGU ATUEPUSHE NAYE.
    KAMA NI UCHU WA MADARAKA HAKIKA MZEE HUYU AMEUBEBEA MBEREKO. JUHUDI ZOTE ZA KUPINGA UFISADI NI UNAFIKI TU YEYE MWENYEWE FISADI. HUYU NDIYE AMEUVURUGA MCHAKATO WA KATIBA MPYA KWA KUSHINDWA KWAKE KULIONGOZA BMK KWA WELEDI, HAKIKA HUYU NI HAINI NAMBA MOJA WA TAIFA LETU NA DAMU YETU HII MIKONONI MWAKE.

  6. Hivi kwani nyie ni akina nani hasa katika nchi hii mpaka mtoe matamko kila wakati kuhusu serikali? Kwani nchi hii ni ya wakristo peke yao? Fanyeni mambo yanayowahusu, inaonekana mnataka kuigawa hii nchi kimisingi ya dini, “ukisema ccm haifuati ushauri wa viongozi wa dini” unamaanisha nini? viongozi wa kiislamu wametoa ushauri wao hapo au mkitoa nyinyi ndio viongozi wa dini? Hubirin habari za Mungu na amani na sio kuvuruga aman, mnatutia wasiwasi sie waumini wenu japo mie ni mkristo-SDA

  7. Kwanza nawapeni pole Viongozi wa Jukwaa la wakiristo Tanzania Kwa ushauri Mzuri lakini Viongozi wetu wametia pamba Masikioni. Haya Wanayaofanya ya kidhalimu yatawahukumu hapa hapa duniani na si muda mrefu. Tatatizo la hawa waheshimiwa wanafikiria kuwa watatawala milele.Nchi ikiwa na kiongozi kama Sitta, tumekwisha hafai kuwa hata kiongozi wa nyumba kumi.Tunaposema wananchi ni pamoja na Viongozi wa dini, namshangaa anayesema waache dini waende kwenye siasa, huyu msamehe maana katumwa na kaingia kichwa kichwa hajui atendalo. Viongozi kaza uzi waelimishe waumini wote wajue haki na wajibu wao katika kuondoa viongozi wasio itakia nchi yetu mema.

  8. ushawai kufika jimbo LA Samuel sitta bac kama haujawai njoo ujionee jimbo lake LA ubunge linaitwa URAMBO ndio utajua unafki WA sitta. Mimi nasema ccm oyee maana wametufumbua macho tuliokuwa tuanazani samwel sitta nimpiganaji na shababi anaefaa kuiongoza nchi. ccm oyee Leo mmempa jukumu LA kupigania maslai ya mwananchi kupitia uundwaji WA katiba mpya yamemshinda anabaki kutapatapa na Mimi naamini samwel sitta moyoni ajutia kujitia kiele-ele kuongoza bunge LA katiba .sasa amekwisha akaongoze kabila lake.

  9. Nadani alichokisema Askofu kina mantiki sana. Wazee wetu akina Salim ahmed salim, Joseph Warioba, Joseph Butiku, Austino Ramadhani sio wapumbavu kiasi hicho kama unavyofikiria. Wanaijua CCM toka enzi za TAA mpaka TANU kwa hiyo walicho kipendekeza kina maana sana. Tunaweza kuchukulia kwa mzaa lakini tutakuja kuikumbuka baadae. Mambo wanoyadai ni muhimu yalisaulika sio kweli kwani hayo yaliachwa makusudi kwa Katiba ya Tanganyika kwa sababu Zanzibar imeyaweka kwenye katiba yake na sio ya Muungano. Kama na madhebu yatatofautiaan ndo hicho tunachokisema katiba haitapatikana kwa kulazimisha na ndo kilio cha wengi kwamba zoezi lisimame kwanza ili tupate muafaka

  10. Simon John,
    angalia maoni yako. Hata askofu ni sehemu ya jamii, siasa isipokwenda vizuri hakuna askofu, hakuna shehe, hakuna amani, hakuna kila kitu. Hivyo kila mtu anayeona siasa haiendi vizuri aweza kutoa maoni yake au ushauri.

  11. Watanzania ni watu wa pekee sana.
    Kuna nukuu moja “Hata kama wananchi watakula maboga, lazima ndege ya rais inunuliwe”. Sasa usemi kama huu una maana kwamba “no one can react on whatever is said by any leader (politician)”. That is what is going on………….

  12. Hongera sana mababa askofu kwa kusema ukweli ubabe wa CCM utaipeleka nchi kubaya viongozi wa dini wana haki ya kuongea. Kuongea ukweli siyo kuingilia siasa kwani siasa nini? kama Sitta anatoa maneno hayo ya dharau kwamba ushauri wa viongozi wa dini hauna utukufu ni dhahiri anaonyesha ubabe na kutaka kuwashurutisha watanzania kuamini kitu ambacho siyo cha kweli Tanzania ni nchi ya watanzania siyo ya CCM -viongozi wa dini wana haki kutoa maoni yao bila kukashifiwa. Maneno hayo ya dharau ya Sitta yanaonyesha wazi kuwa CCM hawana tena nguvu ya hoja wanashindwa kufikiri na kuanza kuweweseka hovyo! Wananchi watashinda tu

  13. CCM! Watanzania wa leo siyo kama wa miaka ya sabini.Maaskofu na voiongozi wote wa dini Tanzania kwa nguvu zote shawishini waumini wenu katiba hii ya SITTA na wanaccm wachache isipite kabisa.Tena tijipange kutafuta namna ya kupambana nao wakitumia ukanjanja wao kuipitisha kihunihuni kama walivofanya

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles