CLARA MATIMO – MWANZA
MASKOFU wa makanisa mbalimbali, wameendelea kuisihi jamii kuepukana na vitendo visivyompendeza Mungu
Wakitoa mahuburi kwa nyakati tofauti j, maaskofu hao walilaani vikali kitendo cha utoaji mimba ambavyo vinaonekana kushika kasi duniani.
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Mwanza, Renatus Nkwande alisema kati ya mwaka 2010 hadi 2014, wastani wa mimba milioni 56 zilitolewa kila mwaka ulimwenguni.
Alisema hayo, ni mauaji makubwa kupiga na ya vita duniani vilivyowahi kutokea duniani kwa sababu ni chukizo mbele za Mungu kwa sababu utoaji mimba kwa makusudi ni dhambi ya mauaji inayolenga kuondoa uhai wa mtoto.
Katika ujumbe wake wa sikukuu ya Krismasi alioutoa kwa waumini kupitia kitabu alichokiandika kuhusu haki na ulinzi wa mtoto chenye kichwa cha habari”Waacheni watoto wadogo waje kwangu”..(Mathayo 19:14) ambacho kilizinduliwa Desemaba 25, mwaka huu katika makanisa yote ya Katoliki Jimbo Kuu la Mwanza na Bunda mkoani Mara.
“Kwa bahati mbaya sana, ulimwengu wa leo unashabikia utoaji mimba na kuna mataifa mbalimbali Ulaya yako nyuma ya dhambi hii ya mauti, yanakazana kutusadikisha Waafrika jambo hili ni zuri…Marekani pekee mwaka 2017, mimba 862,320 zilitolewa, Canada 97, 764 zilitolewa mwaka 2016.
“Mataifa haya, yanatusadikisha tukipunguza idadi ya watu tutapata maendeleo huu ni uongo tu! China ina watu wengi,maendeleo yao mbona yanaenda kasi ya ajabu, tusikubali suala la utoaji mimba katika jamii zetu maana madhara yake ni makubwa mno pia ni dhambi ya mauti inayotupeleka moja kwa moja motoni,”ilieleza sehemu ya ujumbe huo na kufafanua.
“Hivi karibuni watu zaidi ya 1,200 kutoka mataifa mbalimbali wamehudhuria mkutano mkubwa wa kimataifa juu ya idadi ya watu na maendeleo (ICPD25) uliofanyika Nairobi nchini Kenya, mambo ya utoaji mimba na ushoga yalizungumziwa, yakashabikiwa, yakatiliwa mkazo na kuhimizwa.
“Ndugu zangu mambo haya hayatufai katika jamii zetu, tunawashukuru na kuwaombea maaskofu Wakatoliki wa Kenya kupinga kwa nguvu matamko, sera na mipango yote ya kuhalalisha utoaji mimba na ushoga katika jamii zetu ambayo yanapigiwa debe na ICPD 25 maana ni kinyume cha maadili, imani na tamaduni zetu,”.
Askofu Nkwande ambaye pia ni Msimamizi wa Kitume Jimbo la Bunda, aliwataka baadhi ya Waafrika wanaoshiriki kuwadhuru au kuwaua watoto kwa imani za kishirikina, wakiamini wanaweza kupata mali na vyeo waache kwa sababu viungo vya binadamu havileti ustawi wowote wa kiuchumi bali huo ni umaskini wa fikra.
Alisema tendo la kuzaliwa mtoto Yesu katika familia ya Yosefu na Maria, liwakumbushe wakristo kutafakari juu ya haki na ulinzi wa mtoto kama walivyofanya wazazi wake watambue kwamba matendo yote yanayodidimiza haki za mtoto ni kinyume na krismasi.
Nkwande aliahidi kutetea haki ya mtoto ya kuishi tangu siku aliposimikwa rasmi Mei 12, mwaka huu kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza, ambapo aliwataka viongozi wa Serikali nchini kupiga marufuku vitendo vya ushoga na utoaji mimba maana ni machukizo mbele za Mungu.