24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Askofu: Nchi za Afrika zinaongozwa na madikteta

Uju WondersNa SAFINA SARWATT, KILIMANJARO

ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Kipentekoste nchini Nigeria, Uju Wonders, amesema nchi za Afrika zinakabiliwa na changamoto ya kuwa na viongozi madikteta wanaotumia mabavu kuongoza nchi hizo.

Askofu Wonders alitoa kauli hiyo jana mjini Moshi katika kongamano la kimataifa lililoshirikisha madhehebu mbalimbali ya Kikristo barani Afrika, Asia na Ulaya.

Kutokana na uwepo wa viongozi wa aina hiyo, nchi nyingi za Afrika ni masikini kwa kuwa badala ya kuendelea mbele, wamekuwa wakirudishwa nyuma bila wao kutaka.

“Udikteta ndio uliozifikisha nchi za Afrika hapa zilipo. Kwa hiyo ni vema Waafrika wakaamka kutoka usingizini na waungane kwa pamoja ili kuleta mabadiliko katika suala la uongozi.

“Umasikini katika nchi za Afrika hauwezi kuondolewa bila siasa, hivyo ni vema watu wakafanya siasa safi bila kuvunja sheria za nchi kwani viongozi wazuri wanapatikana katika siasa.

“Viongozi wazuri ni wale wenye hofu ya Mungu na uadilifu kwani hao wanasimamia haki na usawa bila ubaguzi wa aina yoyote.

“Pamoja na hayo ni vema Waafrika wakajuana wao kwa wao ili wajadili namna ya kuondokana na utawala wa kidikteta pamoja na umasikini katika bara lao la Afrika.

“Nawaambia kabisa kwamba umasikini  unaoikabili Afrika umetokana na watawala wasiokuwa na hofu ya Mungu, waliojaa uchu wa madaraka na hali hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa maisha duni ya Waafrika walio wengi,” alisema Wonders.

Kwa mujibu wa askofu huyo, ni aibu kwa nchi za Afrika kuomba misaada kutoka mataifa ya Ulaya wakati Bara la Afrika lina rasilimali nyingi zisizokuwa Ulaya.

Naye Mbunge wa zamani wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, alipongeza umoja huo wa Wakristo ulioanzishwa na nchi za Afrika na kusema utasaidia kuwakomboa Waafrika ambao wengi wao ni masikini.

Alitaka pia kongamano hilo litumike kuliombea Taifa ili viongozi waongoze kwa kufuata sheria na Katiba ya nchi.

Naye mwenyeji wa kongamano hilo nchini Tanzania, Askofu Dk. Paul Sixbert, alitaka kongamano hilo litumike kuwabadili viongozi wanaoongoza bila kufuata sheria za nchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles