25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

ARCELONA VS  REAL MADRID: El Classico ya kwanza bila Ronaldo

ADAM MKWEPU NA MITANDAO

MCHEZO wa kwanza wa El Classico wa Ligi Kuu ya Hispania, La Liga, kati ya  Barcelona na Real Madrid tangu kuuzwa kwa Cristiano Ronaldo utachezwa Jumapili ijayo katika Uwanja wa Nou Camp, Barcelona.

Mchezo huo utakuwa wa 10 kwenye ratiba ya La Liga kabla ya kurudiana Machi 3 mwakani mchezo wa 26 katika mzunguko wa pili wa ligi hiyo ambao utachezwa Uwanja wa Santiago Bernabeu.

Lakini kitu pekee katika mchezo huo ni namna utakavyokuwa bila uwepo wa aliyekuwa mshambuliaji wa timu ya Real Mdrid, Ronaldo ambaye Mei mwaka huu alijiunga na Juventus.

Kuondoka kwa Ronaldo  kumepunguza  vita kali iliyokuwapo dhidi ya hasimu wake mkubwa, Lionel Messi anayecheza Barcelona ambaye kwa sasa ni nahodha wa timu hiyo baada ya Andres Iniesta kuondoka.

Kukutana kati ya Barcelona na Real Madrid kwa kawaida hufanya kuwa tamasha la kusisimua, lakini litakuwa kwa mara ya kwanza bila uwepo wa  Ronaldo.

Mchezo wa mwisho ulimalizika timu hizo zikifungana mabao 2-2 baada ya Luis Suarez na Messi  kuifungia Barcelona huku Ronaldo na  Gareth Bale kusawazisha.

Kabla ya mchezo huo Barcelona iliifunga Madrid mabao 3-0 yaliyofungwana na Suarez,  Messi na Aleix Vidal, katika Uwanja wa Bernabeu ambapo beki  wa Real Madrid, Dani Caravajal,  alitolewa uwanjani baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu dakika ya 63.

Barcelona itawakabilia  Real Mdrid ikiwa na tatizo kubwa katika safu ya ulinzi  baada ya kuumia kwa beki, Thomas Vermaelen ambaye atakuwa nje ya uwanja wiki sita akiuguza jeraha la misuli ya paja alilopata akiwa mazoezini.

Timu hizo zitakutana baada ya kucheza dhidi ya Sevilla na  Inter Milan katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Vermaelen anaungana na beki mwingine wa timu hiyo,  Samuel Umtiti, ambaye yupo nje akiuguza majeruhi ya kifundo cha mguu hali ambaye inafanya kocha wa timu hiyo, Ernesto Valverde,  kukuna kichwa wakati akiangalia mapungufu yaliyopo katika safau yake ya ulinzi kikosi cha kwanza.

Umtiti hakucheza tangu September  mwaka huu hata hivyo wiki mbili zilizopita alitakiwa kufanyiwa upasuaji  ambao ungemfanya kuwa nje ya uwanja hadi  mwaka 2019.

Gerard Pique na beki ambaye alisajiliwa katika dirisha la usajili majira ya joto Clement Lenglet, ndio beki pekee wa kati ambao watakuwa katika safu ya ulinzi ya timu hiyo.

Lakini Lenglet, anaonekana bado anahitaji muda zaidi kuzoea mfumo wa timu hiyo wakati Pique  akionekana kufanya makosa kadhaa ya kizembe ambayo huwa yanaigharimu timu hiyo.

Makosa ya kizembe yanayofanywa na beki huyo ndio sababu ya timu hiyo kushindwa kupata ushindi katika michezo minne iliyopita.

Tayari Barcelona  imetikisa nyavu mara tisa katika michezo nane  ya Ligi Kuu Hispania, La Liga sawa na ilivyokuwa msimu uliopita wakati ilipokuwa ikisumbuliwa na eneo la ulinzi.

Jambo jema kwa mashabiki wa Barcelona huenda beki wa kushoto, Sergi Roberto, akapona haraka na kuuwahi mchezo dhidi ya Sevilla iwapo atapona mapema maumivu ya nyuma za paja.

Kama Roberto  atakosa mchezo huo kuna kila dalili akarejea uwanjani katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Inter Milan ambao utachezwa wiki hii.

Dosari nyingine ipo kwa beki, Jordi Alba, ambaye  bado haonekani kufanya vizuri  eneo la beki wa kushoto tangu Lucas Digne kusajiliwa na klabu ya Everton katika usajili wa majaira ya joto yaliyopita.

Katika mfumo wa kutumia mabeki wanne, kocha  Valverde,  huenda akalazuimika kutafuta  beki wengine kutoka kikosi B  au kuingia sokoni ili kuziba mapengo yaliyokuwapo.

Katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, Real Madrid, imeweka rekodi ya kutwaa taji hilo mara tatu mfululizo baada ya kutwaa msimu uliopita.

Lakini imani ya mashabiki wa timu hiyo kwa kocha mpya, Julen Lopetegui, imekuwa dhaifu ukilinganisha na ilivyokuwa kwa aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Zinedine Zidane.

Huu ni mchezo wa El Classico wa 239  kwa timu hizo hata hivyo mchezo wa soka unaonekana kukosa kumbukumbu iwe kwa sasa au kwa wakati uliopita.

Kwa sasa kila mmoja anazungumzia watu waliondoka katika kikosi cha Real Madrid baada ya kufanya vibaya michezo mitatu ya La Liga.

Wiki kadhaa zilizopita Real Madrid ilionekana kucheza kitimu zaidi dhidi ya wapinzani wao Altetico Madrid bila kumtegemea mchezaji mmoja kama ilivyokuwa kipindi cha Ronaldo.

Lakini baada ya kufungwa na  Espanyol  hakuna anayekumbuka  mazuri waliyofanya vijana hao wa Lopetegui dhidi ya Roma katika mchezo wa ufunguzi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya au kukumbuka kuwa timu hiyo inalingana pointi 14 na Barcelona katika  msimamo wa Ligi Kuu Hispania.

Mwaka mmoja uliopita Ronaldo akiwa uwanjani huku Zidane akiongoza benchi la ufundi Real Madrid ilikuwa ikihahaha katika michezo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kabla ya kupoteza mchezo dhidi ya Tottenham Hotspur katika Uwanja wa  Wembley, England na kupitwa pointi saba dhidi ya Barcelona, LaLiga.

Hali hiyo ilitokea katika michuano ambayo Real Madrid ilishinda kwa mara ya tatu mfululizo.

Lakini changamoto  anayokumbana nayo Lopetegui kwa sasa wakati akijiandaa na mchezo El Classico  ni  mashabiki na viongozi wa klabu hiyo kutaka kufanya vizuri kila wakati.

Kitendo cha kushindwa  kufunga katika michezo mitatu iliyopita kimeongeza hofu katika kikosi hicho labda huenda kocha huyo akawa anajadiliwa kufukuzwa.

Kwa sasa kila shabiki ana hoji kuhusu kiwango cha timu hiyo hata hivyo bado wanapaswa kusubiri licha ya kukosa imani naye.

Kivutio pekee katika El Cl;assico ya msimu huu kitahamia  kwa kiungo , Ivan Rakitic  na Luka Modric ambao wanacheza katika timu moja ya taifa la Croatia .

Ratikic amekuwa na kiwango kizuri katika kikosi cha Barcelona tangu arejee akitokea michuano ya Kombe la Dunia hivyo hivyo kwa mwenzake wa Real Madrid ambaye kwa sasa ndio mchezaji bora wa mwaka wa Fifa.

Hii inatokea baada ya miaka kadhaa kupita wakati ushindani ulipokuwa kwa Messi na Ronaldo. Lakini kwa sasa Ronaldo hayupo jambo ambalo linaonekana kuondoa ushindani uliokuwapo hapo awali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles