26.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

ANGELA MERKEL: MWANAMKE MWENYE NGUVU NA USHAWISHI ZAIDI DUNIANI

Na MWANDISHI WETU


KILA mtu akiulizwa ni mwanamke gani maarufu au aliye ngangari zaidi atakuja na jibu tofauti tofauti.

Pengine akitafakari vizuri, anaweza sema ni mama yake, hasa kama alimlea kwa uadilifu na wengine wanaweza kuwataja wake zao kwa kutegemea namna wanavyoishi.

Lakini pia linapokuja suala la mwanamke ambaye hakuhusu, unayeamini ndiye maarufu, mwenye nguvu na ushawishi duniani, hasa katika siasa na uchumi, inaweza kuwa mtihani kutoa jibu sahihi.

Ni kweli, unaweza kutoa jibu, lakini si lazima liwe sahihi.

Kama ni sahihi, itakuwa ni kwa sababu tu, unamjua huyo uliyemtaja na wengine huwajui.

Hivi ndivyo ambavyo imetokea kwenye kura iliyofanyika ya kuwataja wanawake wanaodhaniwa kuwa maarufu duniani.

Kwa mujibu wa jarida maarufu duniani kwa kufanya tathmini za viwango mbalimbali kuanzia utajiri, uzuri na umaarufu wa binadamu, Forbes, Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ndiye mwanamke mwenye nguvu na ushawishi zaidi duniani.

Kansela ametajwa mara sita kushikilia hadhi hiyo tangu alipoingia madarakani miaka 12 iliyopita.

Kwa maneno ya Forbes, Merkel ndiye kiongozi asiyetiliwa shaka wa Umoja wa Ulaya na ni kiongozi wa uchumi halisi duniani.

Anatajwa kama kiongozi wa taifa linaloendesha uchumi wa Ulaya na mwenye ushawishi wa kuamua hatima ya mgogoro mkubwa zaidi wa wakimbizi duniani tangu Vita ya Pili ya Dunia.

Licha ya kuhesabiwa kuwa mwanamke wa shoka na mwanasayansi mpenzi wa soka, ameripotiwa kuwa mwoga mbele ya mbwa.

Aliyekuwa mke wa rais, mgombea urais na Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Hillary Clinton, ameshika namba mbili.

Lakini Merkel ni nani?

Dk. Angela Dorothea Merkel alizaliwa Julai 17, 1954, mjini Hamburg ni mwanasiasa wa Ujerumani ni Kansela wa Ujerumani tangu Novemba 22, 2005.

Licha ya kuzaliwa Hamburg, alikulia katika iliyokuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Ujerumani maarufu kama Ujerumani ya Mashariki, kabla ya Ujerumani zote mbili kuungana na kuwa moja.

Aliishi mashariki mwa Ulaya hadi muungano Ujerumani ulipofanyika mwaka 1990.

Angela Merkel kwa sasa ni mwenyekiti wa chama cha Chama cha Kikristo cha Kidemokrasia cha Ujerumani (CDU).

Mwaka 2009 alitangaza ya kuwa ataachana na Chama cha SPD akitafuta ushirikiano na kile cha FDP.

Uchaguzi wa Bunge wa Septemba 2009 ulirudisha chama chake cha CDU kwa wingi wa viti Bungeni akaendelea kuunda serikali mpya pamoja na FDP.

Tukiachana na hayo, kuna mambo kadhaa ambavyo huenda ukawa huvijui kumhusu ikiwamo kutokuwa na watoto wa kuzaa.

Kasner na familia ya baba yake kwa kiasi fulani wana asili ya Poland.  Merkel ni jina la mumewe wa kwanza aliyekuwa mwanafunzi mwenzake wa Fizikia ambaye waliooana mwaka 1977 na kuachana miaka minne baadaye.

Her Childhood

Baba yake Merkel alikuwa mfanyakazi katika Kanisa la Kilutheri. Alihama na familia yake kutoka Ujerumani Magharibi kwenda Mashariki iliyokuwa ikidhibitiwa na Urusi ya Kisovieti baada ya Angela kuzaliwa huku maelfu wengine wakikimbia.

Nidhamu, uangalifu na umakini wa Merkel katika siasa mara nyingi unaelezwa ulitokana na makuzi yake ya Ujerumani Mashariki.

Alipokuwa na umri wa miaka tisa akiwa katika darasa la gym, aliwahi kupooza kwa dakika 45 akiwa juu ya meza ya kujiandaa kurukia katika bwawa la kuogelea. Mwishowe aliamka na kuruka majini kabla ya darasa kumalizika.

Ana shahada ya fizikia na uzamivu katika kemia na baadhi ya mafanikio yake kama mwanasiasa yanatokana na utaalamu wake wa siasa na uchambuzi wa hali halisi.

Alienda kufanya kazi kama mwanasayansi mtafiti akiwa mwanamke pekee katika kitengo cha nadharia ya kemia katika Chuo cha Sayansi cha Ujerumani Mashariki.

Kufikia mwishoni mwa 1970, Merkel aliomba kazi ya profesa msaidizi katika shule ya uhandisi na alitakiwa kujiunga na  Stasi, yaani polisi wa siri wa Ujerumani Mashariki.

Hata hivyo, alikataa kujiunga na kikosi hicho kilichoogopewa, akidai atakuwa mpelelezi mbaya kwa vile ana mdomo kama kasuku.

Hivyo, akakosa kazi lakini pia iwapo angejiunga na polisi hao, asingefikia hapo alipo kisiasa.

Yaani iwapo angejiunga nacho, hatima ya baadaye ya kisiasa ingekuwa ngumu, kwa vile wanasiasa wa Ujerumani iliyoungana waliokuwa na uhusiano ya nyuma na Stasi walihesabiwa sumu kali na wengi walilazimika kujiuzulu baada ya kubainika uhusiano wao nao wa nyuma.

Baada ya Merkel kutengana na mumewe wa kwanza, akaishi kama mtu asiye na makao maalumu akijikunyata katika makazi haramu karibu na stesheni ya reli ya Friedrichstrasse.

 Wakati wa siku yake ya 30 kuzaliwa akionekana kana kwamba anaelekea kupotea, baba yake alimtembelea na kumwambia ‘hujachelewa bado kujirudi.”

Usiku mmoja ukuta wa Berlin ukaangushwa ile Novemba 1989, akiwa na umri wa miaka 35 alitembelea sauna.

Baada ya kuranda randa mpakani na wengine akipoza koo kwa chupa moja ya bia mara moja alirudi nyumbani ili asijichokee kwa kazi ya siku iliyofuata.

Karibu kila Mjerumani alikuwa mtaani usiku mwingi kusherehekea tukio hilo.

Mumewe wa sasa Joachim Sauer, profesa wa chuo Kikuu cha Berlin anachukia kumulikwa hadharani na hivyo huwa hajitokezi katika matukio mengi ikiwamo wakati wa alipoapishwa kwa mara ya kwanza ukansela mara ya kwanza mwaka 2005.

Mumewe huyo anajulikana kwa kubana matumizi ikiwamo kupanda ndege za gharama nafuu hata kama anaruhusiwa kusafiri na mkewe katika ndege rasmi.

Hupenda kuangalia maonesho na kutembea pamoja.

Merkel ameripotiwa kuwa mpishi mzuri na mtaalamu wa kutengeneza kesi na amekuwa akionwa akinunua katika groceries katika maduka makubwa ambako hulipa pesa tasilim. Na alimwambia Rais wa zamani wa Nigeria Goodluck Jonathan kuwa humwandalia mumewe kifungua kinywa kila asubuhi.

Ni mwoga wa mbwa baada ya kuwahi kung’atwa mwaka 1995, kitu kinachodaiwa kumfanya Rais wa Urusi Vladimir Putin mara kwa mara kutumia mbwa wake kujaribu kumwongopesha

Mara kwa mara huingia katika vyumba vya kubadilisha nguo vya timu za soka na kupongeza wachezaji na aliwahi kumshuhudia nyota wa Ujerumani Bastian Schweinsteiger akiwa mtupu kama aliovyozaliwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles