24.4 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

ANC WAKOLEZA MOTO KUMNG’OA ZUMA

JOHANNESBURG, AFRIKA KUSINI


KAMATI ya Maadili (IC) ya Chama Tawala cha African National Congress (ANC), imependekeza kufukuzwa kwa Rais Jacob Zuma.

Aidha kikao hicho kilichoitishwa kwa dharura kumjadili Zuma, kilitoa waraka maalumu kuhusu utendaji kazi wa kiongozi huyo.

Waraka huo uliosainiwa na Mwenyekiti wa IC, Andrew Mlangeni, ulipangwa kuwasilishwa kwa Katibu Mkuu wa ANC, Gwede Mantshe, ambaye ameombwa kuitisha mkutano wa dharura kujadili mwenendo wa Rais Zuma.

Katika waraka huo, Mlangeni alisema kamati hiyo imevunjwa moyo kwa jinsi Rais Zuma alivyochukua uamuzi wa kulifanyia mabadiliko Baraza la Mawaziri bila kushauriana na upande wowote.

Vyanzo vya habari vinasema IC imepanga kukutana na Rais Zuma mwishoni mwa wiki kumshinikiza aachie ngazi.

Hatua ya hivi karibuni ya Rais Zuma kumfuta kazi Waziri wa Fedha, Pravin Gordham, imezusha mzozo ndani ya ANC huku thamani ya fedha – Rand ikiendelea kuporomoka.

Makamu wa Rais, Cyril Ramaphosa, alikosoa uamuzi huo akisema hakubaliani nao.

Vyama vikuu vya upinzani kama Democratic Alliance (DA) na Economic Freedom Fighters Party (EFF), vimemwandikia barua Spika wa Bunge la Afrika Kusini, Baleka Mbete vikimtaka aitishe kikao cha dharura cha Bunge kujadili suala hilo.

Kikao cha awali kilichoitishwa na Bunge la Afika Kusini kupiga kura ya kutokuwa na imani na Rais Zuma, kilishindwa kutokana na idadi kubwa ya wawakilishi wa ANC bungeni.

Hata hivyo, huenda safari hii hali ikawa tofauti kutokana na kukithiri kwa kashfa za Rais Zuma na hali ya mpasuko inayoendelea kushika kasi ndani ya chama chake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles