Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
Kampuni ya Simu za Mkononi ya Airtel, imezindua huduma mpya ya kutuma na kupokea fedha kupitia Airtel Money bila makato.
Mkurugenzi wa Masoko wa kampuni hiyo, Isack Nchunda amesema hayo leo Alhamisi Julai 5, na kuongeza kuwa lengo la huduma hiyo inayojulikana kama ‘Hakatwi Mtu Hapa-Tuma Pesa Bure’ ni kuunga mkono juhudi za serikali na kuwawezesha wateja wa Airtel nchini kutuma na kupokea fedha bure.
“Mwaka jana tulizindua huduma ya kutuma na kupokea fedha bure kwa wateja wa Airtel Money wanaotuma fedha kuanzia sh 200,000 na kuendelea na sasa tumezingatia tena uhitaji wa huduma kwa wateja wetu wengi kupitia huduma hii ambayo tunaamini watakaoitumia wataifurahia.
“Tunategemea kuona wateja wakichangamkia fursa hii ya kutuma na kupokea fedha bila makato yoyote ili kuokoa fedha zaidi ya Sh 5,000 kuanzia sasa,” amesema.
Pamoja na mambo mengine, Nchunda amesema Airtel imelenga kuboresha huduma za kifedha nchini kwa kuwafikia zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania ambao hawajafikiwa na huduma za kibenki ambapo imeunganishwa na benki zaidi ya 40 ili kurahisisha wateja kufanya mihamala mbalimbali kama vile kuhamisha fedha kutoka kwenye akaunti ya benki kwenda kwenye akaunti ya Airtel Money muda wowote.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Airtel, Beatrice Singano amesema huduma hiyo ni rahisi na inapatikana kwenye maduka zaidi ya 50,000 ya Airtel nchi nzima.
“Kupitia huduma hii mpya, wateja wetu wataweza kuokoa zaidi ya Sh 5,000 ya kutuma fedha ambayo kwa mwananchi wa kawaida ni fedha nyingi inayotosheleza mahitaji ya siku,” amesema.