23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Afrika yatakiwa kuandaa rasilimali watu

Na NORA DAMIAN

-DAR ES SALAAM

NAIBU Balozi wa Japan, Katsutoshi Takeda, amesema mataifa ya Afrika yanatakiwa yaandae rasilimali watu watakaoweza kusimamia na kuendeleza sekta mbalimbali ili kuleta tija kwa taifa husika.

Akizungumza jana wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya uongozi na usimamizi wa rasilimali watu, Balozi Takeda alisema utoaji mafunzo hayo ni njia bora ya kuwekeza katika rasilimali watu.

Mafunzo hayo yaliyoshirikisha washiriki kutoka taasisi za umma na binafsi yameandaliwa kwa ushirikiano wa Taasisi iliyo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara Japan inayojihusisha kutoa mafunzo ya uongozi na utawala (AOTS) na taasisi ya hapa nchini inayojihusisha kutoa mafunzo ya namna hiyo (OTIDE).

“Mafunzo haya yakitumika vema yatakuwa ni tija kubwa kwa kusukuma maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika nchi nyingi,” alisema Balozi Takeda.  

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Godfrey Simbeye, alisema bila ujuzi nchi haitaweza kufanikiwa kuingia kwenye uchumi wa viwanda hivyo mafunzo hayo ni muhimu.

Alisema katika kuunga mkono mkakati wa kitaifa wa kukuza ujuzi ambao ulianza 2016 – 2026/27, wanatarajia kuanzisha mabaraza ya ujuzi ya kisekta ambayo yatazinduliwa mwezi huu.

“Sisi tunadhani semina hizi zitasaidia kukuza ujuzi, tunachohitaji ni mabadiliko kwenye sehemu zetu za kazi, kuongeza utendaji ulio na tija zaidi tuweze kufanya mambo yetu kwa haraka,” alisema Simbeye.

Awali Mwenyekiti wa OTIDE, Hamadi Mwinyikondo, alisema mafunzo hayo ambayo yanafanyika kwa mara ya kwanza hapa nchini yanalenga kuinua uzalishaji kwenye taasisi za umma na binafsi.

Alifafanua kuwa OTIDE inaundwa na Watanzania ambao waliwahi kupelekwa Japan na kusomeshwa na taasisi ya AOTS na kwamba huwa wanapendekeza kila mara aina ya mafunzo ambayo yatasaidia kuwaongoza watu ili utendaji wao wa kazi usababishe uzalishaji zaidi.

“Mafunzo haya yamejikita kwenye mambo makubwa mawili, uongozi wa taasisi na usimamizi wa rasilimali watu, kwa maana ya namna ya kuongoza watu, kutatua migogoro mahala pa kazi, kunyanyua hari ya rasilimali watu ili kuongeza uzalishaji,” alisema Mwinyikondo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles