24.4 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

ACT – Wazalendo yatabiri uchumi kuporomoka

Pg 3NA WAANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

CHAMA cha ACT – Wazalendo kimesema katika kipindi cha miezi sita tangu Serikali ya awamu ya tano iingie madarakani, uchumi wa taifa umeporomoka kwa asilimia nne.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Kiongozi Mkuu wa chama hicho, Zitto Kabwe, akinukuu taarifa ya Benki Kuu (BOT), alisema katika kipindi cha Oktoba hadi Desemba mwaka jana, pato la taifa lilikua kwa asilimia tisa. Lakini kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu, limepungua na kufikia asilimia 5.5.

Alisema kulingana na mwenendo wa uchumi, Kamati Kuu ya chama hicho imeitaka Serikali izingatie sayansi ya uchumi katika kuendesha nchi.

Zitto alisema uamuzi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa kuitelekeza Serikali kwa mwanasiasa mmoja na kudhani ndiye anayejua kila kitu na kuwa mshauri wa washauri wa uchumi, itasambaratisha uwekezaji nchini na kuua kabisa juhudi za miaka 20 za kuvutia uwekezaji na kujenga uchumi shirikishi.

“Tunawahimiza wananchi kuzingatia kuwa msingi wa uchumi wetu ni uwekezaji kutoka ndani na nje ya nchi, hivyo msingi wa kuvutia uwekezaji ni utawala bora. Serikali ya CCM inapaswa kujua kuwa kuua utawala wa sheria ni kuua uwekezaji pamoja na uchumi wa nchini.

“Tangu kuingia kwa awamu ya tano, Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi imekumbana na changamoto ya uchumi kukua bila kuwanufaisha wananchi wa kawaida, wakati tulitegemea Serikali mpya ingeanza na kukuza uchumi wa taifa.

“Hali hiyo inamaanisha kuwa ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika kipindi cha miezi sita ya mwanzo wa  awamu ya tano umepungua kwa asilimia 4,” alisema Zitto.

Zitto ambaye alikuwa akitoa msimamo wa Kamati Kuu ya chama chake iliyoketi juzi Dar es Salaam, alisema katika sekta ya kilimo ambayo hutegemewa na wananchi kwa asilimia 70, pato la uchumi limezidi kushuka kutoka kasi ya ukuaji wa asilimia 10 kwa robo ya mwisho wa mwaka jana hadi kufikia asilimia 2.7 katika kipindi cha Januari hadi Machi, mwaka huu.

“Watu wameishiwa na imani kuendelea na shughuli za ujenzi, mfano nyumba zilizokuwa zikijengwa zimeachwa kujengwa,” alisema.

Habari hii imeandaliwa na Herieth Faustine, Johanes Respichius na Pauline Kebaki (Turdaco).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles