27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

ACACIA WAKIRI  MAKINIKIA YAMEWATIKISA

Na HARRIETH MANDARI

-GEITA

KAMPUNI ya uchimbazaji dhahabu katika Mgodi wa Bulyanhulu Acacia imesema uamuzi wa Serikali kuzuia usafirishaji wa makinikia nje ya nchi kumewasababishia hasara kubwa, hivyo wameufunga mgodi kutokana na kupanda kwa gharama za uzalishaji.

Meneja Mkuu wa Uhusiano wa kampuni hiyo, Asa Mwaipopo alisema mgodi wa Bulyanhulu (BGML), umepoteza nusu ya mapato yake yote ya awali.

Akizungumza katika hafla ya kuwaaga wafanyakazi wa mgodi huo juzi, Mwaipopo alisema uzalishaji katika mgodi huo umepungua kutoka wakia 300,000 hadi aunzi 2,000 kwa mwezi kiasi ambacho alidai ni kidogo na hakina faida yoyote kwa kampuni.

Mwaipopo alisema hatua hiyo imechukuliwa kutokana na kupungua kwa uzalishaji, hivyo kufanya mgodi huo kushindwa kumudu gharama za uendeshaji.

Alisema kutokana na hilo Septemba 15 wamefikia uamuzi wa kupunguza rasmi shughuli za uzalishaji sambamba na wafanyakazi 150 akiwamo aliyekuwa Meneja Mkuu wa mdogi huo, Graham Crew ili kuepuka hasara zaidi.

“Tumepata hasara kimapato ambayo ni chini ya nusu ya mapato yetu, tumekuwa tukilazimika kutumia akiba ya fedha iliyokuwepo kwa ajili ya kuendesha mgodi na kulipa wafanyakazi,”alisema.

Kwa upande wake, Crew alisema tangu kuanza kwa shughuli za uchimbaji na uzalishaji dhahabu katika mgodi huo wamewekeza zaidi ya Sh trilioni 8 huku matumizi yakiwa ni Sh trilioni 6.6 na kodi mbalimbali zikigharimu Sh trilioni 2.2.

Aidha katika kuwaandaa wafanyakazi hao, alisema wamekutana mara ikiwa ni pamoja na kuwaeleza kutokata tamaa ya maisha baada ya kuondoka mgodini hapo na kuwataka kutumie vizuri elimu ya ujasiriamali waliyoipata kujikimu kiuchumi.

“Wafanyakazi mpeta elimu ya ujasiriamali, nimewaeleza kasimame imara, muwe tayari kukabiliana na maisha nje ya mgodi kwani maisha siyo mgodini pekee yapo hata nje ya hapa…, inawezekana kabisa kufanya shughuli zingine za kiuchumi na maisha yakaendelea,”alisema Crew.

Kuhusu hatima ya mgodi huo, Crew alisema kuwa watabakia wafanyakazi wachache ambao wataendelea na uchenjuaji wa dhahabu kwa kutumia tope la makinikia hivyo kuzalisha miche ya dhahabu.

“Mgodi huu bado utaendelela kutoa kodi ya huduma kwa asilimia 67 ambayo ni sawa na Sh milioni 176  ambacho hutolewa kwa Wilaya ya Msalala, asilimia 33 na Wilaya ya Nyanghwale ambayo ni sawa na Sh milioni 87,” alifafanua.

Hatua ya kufungwa kwa migodi hiyo inatokana na kile wanachodai kupinga uamuzi wa kamati za uchunguzi zilizoundwa Rais Dk. John Magufuli kuchunguza usafirishaji wa mchanga wa dhahabu na masuala ya kiuchumi na kisheria.

Ripiti za kamati hiyo ziliibuka masuala mazito ikiwemo  kutosajiliwa kwa kampuni ya Acacia Mining inayojinasibisha kuwa mmiliki wa kampuni za Bulyanhulu Gold Mines, North Mara Gold Mine na Pangea Minerals.

“Kamati imebaini na kuthibitisha kwa mujibu wa nyaraka na maelezo kutoka ofisi ya msajili wa makampuni (Brela) kuwa kampuni ya Acacia Mining Plc haikusajiliwa nchini Tanzania na wala haina hati ya utambuzi kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni, Sura ya 212,” alisema Profesa Osoro.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles