30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

ABIRIA WANAOTAPELIWA HUPONZWA NA KUPENDA UNAFUU – MWALONGO

Na CHRISTINA GAULUHANGA-DAR ES SALAAM


UWAPO wa wapiga debe katika vituo mbalimbali vya mabasi, umekuwa ukichangia kuleta kero kwa abiria na kuhatarisha usalama wa maisha yao pamoja na mali zao.

Serikali kwa muda mrefu imekuwa ikisisitiza matumizi ya mfumo wa kieletroniki ili kuondoa adha mbalimbali ikiwamo usumbufu wa kuuzia tiketi hewa au bei juu.

Ni kwa muda mrefu wapiga debe wamekuwa chanzo cha vurugu katika vituo vya mabasi huku wakisabisha adha kwa abiria wanaotumia vituo hivyo au wapita njia.

Mkazi waTabata Relini, Saida Husein, anasema ni vyema mamlaka zinazosimamia usafiri nchini zikazingatia sheria ya usalama barabarani kama Mamlakka ya Usimamizi Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra).

Anasema endapo wamiliki wa mabasi wataimarisha mfumo wa ukataji tiketi kwa njia ya kieletroniki, itasaidia kuwapunguza wapiga debe vituoni na kuimarisha huduma ya usafiri.

Saida anasema endapo wamiliki watazingatia matumizi sahihi ya mfumo wa kielektroniki katika ukatishaji tiketi itasaidia kuwapunguzia adha wasafiri mara wanapohitaji huduma ya tiketi.

“Baadhi ya wamiliki wa mabasi wanaweza wakawa chanzo cha vurugu katika vituo vya mabasi kwa kuwa kitendo cha kuendelea kutoa fedha kwa wapiga debe kunaimarisha mizizi ya uwapo wa kundi hilo vituoni,” anasema.

Anawashauri wasafiri kuwa makini pindi wanapouziwa tiketi nje ya ofisi za mabasi kwa sababu zimekuwa zikisababisha kero kwa abiria na udanganyifu.

Ofisa Habari wa Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa), Mustapha Mwalongo, anasema ili kuondoa adha ya kuuziwa tiketi feki au kupandishiwa gharama halisi ni vyema abiria wakajenga mazoea ya kwenda moja kwa moja kwenye ofisi za mabasi husika.

Anasema shida ni kwamba baadhi ya abiria wamekuwa wakipenda gharama nafuu, hivyo hutafuta tiketi za bei nafuu jambo ambalo huwafanya watapeliwe.

Kwa upande wake Ofisa Habari wa Elimu kwa Umma wa Baraza la Ushauri Watumiaji Huduma za Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra CCC), Nicholous Kinyariri, anasema wao wana wajibu wa kuwakumbusha watumiaji huduma za usafiri kutambua wajibu wao.

Anasema abiria anapotaka kusafiri ni vyema akafanya maandalizi mapema ili kuepuka usumbufu.

Kinyariri anasema abiria anapaswa kukumbuka kuwa tiketi ina umuhimu katika safari yake yoyote ili iweze kumlinda mara inapotokea ajali au gari kuharibika.

“Wapo baadhi ya watu wamejenga mazoea ya kusafiri bila tiketi jambo ambalo limekuwa likiwanyima haki zao za msingi ikiwamo matibabu na ulipwaji fidia pindi ajali inapotokea.

Kinyariri anasisitiza abiria kulipa nauli, kupata tiketi na kuzingatia usalama wake pindi anapokuwa safarini, akiona dereva anaendesha mwendokasi au wahudumu wa gari kutumia lugha chafu ni vyema wakatoa taarifa mapema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles