30.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 30, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali kuchunguza ukarabati shule kongwe

Na DERICK MILTON-MASWA

SERIKALI imesema kuwa itafanya uchunguzi wa matumizi ya fedha ambazo zinapelekwa kwenye shule kongwe za sekondari ambazo zinakarabatiwa kutokana na kuwepo kwa matumizi mabaya ya fedha hizo.

Hatua hiyo ya serikali imekuja baada ya kubaini uwepo wa matumizi mabaya ya fedha hizo kwa baadhi ya shule ambazo zimepelekewa pesa hizo ili zikarabatiwe huku maeneo mengine ikisababisha migogoro kati ya walimu na uongozi wa shule.

Kauli hiyo imetolewa jana na Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Mwita Waitara, baada ya kukagua ukarabati wa shule ya Sekondari ya Wasichana Maswa mkoani Simiyu.

Waitara alisema kuwa baadhi ya shule zilizofanya ukarabati huo, majengo yake yameanza kuharibika kwa muda mfupi tangu ujenzi wake ukamilike jambo linalochangia na kutokuwapo matumizi bora ya fedha hizo.

Alisema kuwa serikali imetoa fedha hizo na kuelekeza zitumike kwa mfumo ‘force account’, ambapo shule husika ujiwekea utaratibu zenyewe wa kutafuta mafundi wa kufanya ukarabati huo na kununua vifaa yenyewe.

Alisema kuwa moja ya shule hizo ipo katika Mkoa wa Morogoro Wilaya ya Kilombero, ambapo wamekuta kuna matumizi mabaya ya fedha hizo ikiwemo migogoro kati ya mkuu wa shule na walimu.

“Ujenzi ukikamilika tunakuja kufanya uchunguzi kujilidhisha kama kuna kuna matumizi sahihi ya pesa za serikali, kule Ifakara mkuu wa shule tumemwondoa maana tumekuta mgogoro mkubwa ambao umesababishwa na fedha hizo na kuna matumizi mabaya,” alisema Waitara.

Naibu Waziri huyo alizitaka shule zote ambazo zinafanya ukarabati huo kuhakikisha wanatumia vyema fedha hizo kama inavyotakiwa kwa kushirikisha kila mdau wakiwemo watalaamu wa halmashuari ujenzi.

Akiwa katika Kijiji cha Mwadila Shule ya Sekondari Sukuma alikagua ujenzi wa vyumba vya madarasa,  ambapo aliwataka viongozi ngazi za vijiji na kata kutotumia nguvu katika kuwalazimisha wananchi kuchangia ujenzi huo.

Awali akitoa taarifa ya ukarabati wa shule hiyo ya Wasichana ya Maswa, Mkuu wa shule hiyo, Kuyunga Jackson alisema kuwa walipokea kiasi cha Sh milioni 883, kutoka serikalini na ukarabati umefikia asilimia 75 na utakamilika Januari, 30 2019.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles