33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali yaimarisha udhibiti teknolojia ya nyuklia


Na MWANDISHI WETU-ARUSHA

SERIKALI kupitia Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), imesema kuwa imefanikiwa kuimarisha usimamizi na udhibiti wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia nchini.

Hayo yamesemwa jana na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William ole Nasha wakati akifungua mkutano wa kimataifa wa waratibu wa miradi ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kutoka nchi 46 wanachama wa Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki (IAEA) unaofanyika jijini hapa.

Ole Nasha alisema shirika hilo linafadhili miradi mingi katika sekta mbalimbali hapa nchini ikiwemo sekta ya afya.

Alisema shirika hilo limewezesha kupatikana kwa vifaa mbalimbali vya uchunguzi wa tiba na maradhi ya saratani, ambavyo vimefungwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa Bugando jijini Mwanza na Hospitali ya Ocean Road jijini Dar es Salaam.

Pia taasisi nyingine mbalimbali zimepata vifaa vya maabara na vyote kwa ujumla wake vina thamani ya Sh bilioni 6.2.

Shirika hilo pia limetoa mafunzo kwa wataalamu katika eneo  la matumizi ya mionzi na teknolojia ya nyuklia mpango ambao uligharimu Sh bilioni 3.3.

“Majadiliano yenu yalenge katika kuhakikisha mionzi na teknoljia ya nyuklia katika Afrika inatumika vizuri kwa maendeleo,” alisema Nasha.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa IAEA, Profesa Shaukat Abdulrazak, alisema wataendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha matumizi salama ya teknolojia ya nyukilia kwenye sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, mifugo, maji, viwanda na ujenzi.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Nguzu za Atomiki Tanzania, Profesa Lazaro Busagara, alisema taasisi yake imeendelea kudhibiti na kuwachukulia hatua ya kuzifungia taasisi zinazokiuka taratibu za matumizi salama ya mionzi na teknolojia ya nyuklia hapa nchini ikiwemo kutokuwa na leseni, kutokuwa na wafanyakazi wenye utaalamu wa matumizi ya mionzi na teknolojia.

Alisema mwaka jana walifungia hospitali 112 zilizoshindwa kufuata masharti hayo, katika hizi tayari 40 zimekidhi na kufunguliwa huku 72 zikiwa bado zimefungiwa kutumia vifaa vinavyotumia mionzi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles