25.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

NSSF yaanza kutekeleza agizo la JPM

LEONARD MANG’OHA-DAR ES SALAAM

MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), umeanza kutekeleza maagizo ya Rais Dk. John Magufuli wa kulipa mafao ya wastaafu kwa kutumia utaratibu wa zamani alioutoa Desemba 28, mwaka jana wakati wa mkutano na vyama vya wafanyakazi.

Katika mkutano huo, ulioshirikisha watendaji wakuu wa mifuko ya hifadhi ya jamii, Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) na Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Rais Dk. Magufuli aliitaka mifuko yote ya hifadhi ya jamii kuendelea kutumia kikokotoo kilichokuwa kikitumika awali kabla ya mifuko hiyo kuunganishwa na kutoa kipindi cha mpito hadi 2023.

Pia aliiagiza mifuko hiyo kuendelea kutoa asilimia 50 ya mafao ya kustaafu kwa mkupuo na asilimia 50 kama pensheni ya kila mwezi na badala ya mfumo mpya unaopendekeza kulipa asilimia 25 kwa mkupuo na asilimia 75 kila mwezi kama pensheni

Dk. Magufuli aliwaagiza wenyeviti na watendaji wakuu wa mifuko ya hifadhi ya PSSSF na NSSF, Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu kusimamia mchakato wa kuhakiki majina ya wastaafu ili kupata wastaafu hewa.

Maagizo hayo ni pamoja na mifuko hiyo kupunguza matumizi aliyoyaita ya ovyo, kuhakiki daftari la wastaafu, kuepuka uwekezaji usio na tija kama unaonufaisha watu binafsi na kupunguza gharama za uendeshaji wa mifuko hiyo kwa sababu imebaki miwili hivyo hakuna ushindani na kila mmoja ana wanachama wake.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Meneja Kiongizi wa Matekelezo wa mfuko huo, Cosmas Sasi alisema kwa sasa wanaendelea kupokea na kuhakiki madai ya kutoka kwa wanachama waliokuwa kwenye ajira za muda maalumu.

“Wanachama hao ni ambao ajira zao zimekoma na walikuwa kwenye ajira za muda maalunu kwenye sekta mbalimbali kama madini, viwanda, ujenzi na kilimo na nyinginezo. Madai yote yanayothibitishwa ni halali, baada ya kuhakikiwa mwanachama atalipwa mafao yake” alisema Sasi.

Alisema kuanzia Julai mwaka jana mfuko huo umekuwa ukilipa Sh bilioni tano kila mwezi kwa wastaafu kuanzia Julai mwaka jana kama pensheni ya kila mwezi.

“Kwa pensheni ya  Desemba, 2018, kiasi cha Sh bilioni 4.83 kimeshalipwa kwa wastaafu 18,631 waliokuwapo kwenye daftari la wastaafu walilipwa Sh bilioni 4.83,

“Kwa upande wa malimbikizo ya mafao hadi Julai mwaka jana jumla ya Sh bilioni 108 zilikuwa zinadaiwa kwenye shirika, ambapo kiasi cha Sh bilioni 85 kimelipwa kwa wanachama waliokuwa na madai mbalimbali baada ya uhakiki kukamilika. Kiasi cha Sh bilioni 23 kilizobaki kitalipwa baada ya uhakiki unaoendelea kukamilika” alisema Sasi.

Naye Meneja Kiongozi wa Uhusiano na Elimu kwa Umma wa mfuko huo, Lulu Mengele, alisema mfuko huo umekuwa katika uhakiki wa wastaafu tangu Desemba Mosi mwaka jana katika ofisi zake zote za mikoa na utaendelea hadi Januari 31 mwaka huu.

Lulu, aliwataka wastaafu ambao hawajafanyiwa uhakiki kujitokeza kuhakiki taarifa zao katika ofisi zilizo karibu yao na kwamba watakaoshindwa kufanya hivyo hadi mwisho wa mwezi huu wataondolewa kwenye orodha ya malipo pensheni.

“Kazi yaa uhakiki litakuwa endelevu ili kuboresha taarifa zilizopo kwenye daftari la wastaafu. Shirika linasisitiza wafanyakazi na maofisa utumishi kuhakikisha madai yanayoletwa kwenye mfuko ni sahihi na mtu atakayebainika kuleta madai ya kugushi atachukuliwa hatua za kisheria ikiwamo kupelekwa mahakamani kwani hilo ni kosa la jinai” alisema Lulu.

Kuhusu fao la kupoteza ajira, Lulu alifafanua kuwa wafanyakazi waliokuwa na ajira za muda mfupi wasiokuwa wanataaluma watalipwa mafao yao yote na hawatalazimika kusubiri hadi miaka 55 ya kustaafu.

“Kwa watu kama wahasibu na madaktari ambao wana uwezokano wa kupata kazi tena tunawapa 1/3 ya mishahara yao kwa miezi sita na endapo atapata kazi tutaendelea naye kama mstaafu atakayestaafu kisheria kwa miaka 55” alifafanua Lulu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles