30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Shein: Fanyeni kazi kwenye mazingira bora

MWANDISHI WETU-ZANZIBAR

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa miongoni mwa malengo makuu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuona kwamba watumishi wa umma wanafanya kazi zao wakiwa katika mazingira yaliyo bora na salama zaidi.

Dk. Shein aliayasema hayo jana katika hafla ya uzinduzi wa Jengo la Ofisi za Serikali huko Gombani Chake Chake Pemba, Mkoa wa Kusini Pemba, ambapo viongozi mbali mbali wa vyama na serikali pamoja na wananchi na wafanyakazi walihudhuria.

Alisema kuwa uzinduzi wa jengo hilo ni miongoni mwa vielelezo muhimu vya utekelezaji wa lengo hilo kwani majengo ya ofisi ndio mahali pa kufanyia kazi ambapo hutumia muda mwingi ambayo ni theluthi moja ya siku nzima baada ya kutoka nyumbani.

Alieleza kuwa kuwa na mahala pazuri pa kufanyia kazi kunampelekea mtendaji afanye kazi kwa furaha, umakini na kujiamini Zaidi na ndio maana Serikali imeamua kujenga.

Aliongeza kuwa ujenzi wa jengo hilo ni jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia maamuzi ya Baraza la Mapinduzi ambapo hatua yote hiyo ni kuwawwzesha wafanyakazi katika mazingira mazuri.

Alieleza kuwa ujenzi huo unatokana na baadhi ya ofisi kuchakaa, nyengine hazina nafasi ya kutosha kwa ajili ya watumishi pamoja na wananchi wanaofika kwa ajili ya kupatiwa huduma.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa baadhi ya wizara na taasisi nyingine za Serikali zililazimika kukodi nyumba kutokana na uhaba wa majengo halisi ya kiofisi hali ambayo haipendezi hivyo Serikali itaendelea kujenga majengo ya ofisi Unguja na Pemba.

“Serikali imejenga ofisi hizi ili kurahisisha utoaji wa huduma hivyo, kila mfanyakazi ahakikishe kwamba anawajibika ipasavyo kulingana na dhamana na majukumu ya kazi aliyopangiwa,” alisema Dk. Shein

Aliwataka wafanyakazi wahakikishe wanatumia vizuri muda wa kazi kwa kufanya mambo yanayopaswa kufanywa katika sehemu za kazi.

Alisisitiza wafanyakazi kufanya kazi kwa masaa manane ya kazi kwa siku kwani hatua hiyo itaongeza ufanisi na kuongeza mapato huku akisisitiza haja kwa wafanyakazi kutunza siri za kazi kwani nyenzo kubwa katika utawala bora sambamba na kujiepusha na malumbano.

 “Wafanyakazi wanatumia muda mwingi kazini kuchati na kuperuzi katika mitandao ya kijamii vile vile natoa indhari kwa wale wanaotega kazi kwamba kuwepo kwa ofisi hizi ndani ya jengo moja kusichukuliwe kuwa ni ukaribu wa marafiki kuonana kirahisi kwa ajili ya mazungumzo,” alisema Dk. Shein.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles