23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Azam FC yaididimiza Africa Lyon

THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

TIMU ya Azam FC imeifunga African Lyon mabao 3-1, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara na kuzidi kushikilia nafasi yake ya pili kwenye msimamo wa ligi hiyo.

Azam FC kwa sasa wananolewa na makocha Meja mstaafu Abdul Mingange na Idd Cheche, walianza kwa kasi mchezo huo, ambapo katika dakika ya sita, walipata bao la kwanza lililofungwa  kwa kichwa na Obrey Chirwa, akiunganisha pasi ya Ramadhan Singano.


Hata hivyo, African Lyon walijitutumua na kusawazisha bao hilo katika dakika ya 15, kupitia kwa Baraka Jafary.

Azam FC waliendelea kuliandama lango la African Lyon mara kwa mara, huku wakisaka mabao zaidi.

Katika dakika ya 19, Salum Abubakar ‘Sure Boy’ alipiga shuti na mpira kutoka nje.

African Lyon waliweza kuhimili vishindo na katika dakika ya 44, Benedictor Jacob alipiga shuti lililookolewa na mabeki wa Azam FC.

Timu hizo zilikwenda mapumziko huku zikiwa zimetoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1.

Kipindi cha pili kilianza huku Azam FC wakifanya mabadiliko kwa kutoka Tafadzwa Kutinyu na Frank Domayo na nafasi zao kuchukuliwa na  Stephen Kingue na Donald Ngoma.

Mabadiliko hayo yaliongeza mashambulizi kwa Azam FC ambapo katika dakika ya 57, Donald Ngoma aliambaa na mpira, lakini alishindwa kufanya maamuzi na mpira kuokolewa na mabeki wa African Lyon.

Katika dakika ya 64, Mudathir Yahya aliipatia Azam FC bao la pili baada ya kuachia shuti kali lililomshinda kipa wa African Lyon, Douglas Kasembo.

Baada ya kuingia bao hilo, Azam FC walifanya mabadiliko katika dakika ya 65 kwa kumtoa Ramadhan Singano na kuingia Danny Lyanga.

Azam FC waliendelea kuliandama lango la African Lyon na katika dakika ya 89, Bruce Kangwa aliipatia timu yake bao la tatu baada ya kupiga krosi na beki wa kujifunga.

Hadi dakika 90 za mchezo huo zinamalizika, Azam FC ilitoka kifua mbele kwa ushindi huo wa mabao 3-1 na hivyo kuendelea kufufua matumaini ya kuwania ubingwa huo, ikiwa nafasi ya pili kwa kujikusanyia pointi 53, katika michezo 26 iliyocheza.

Azam FC inazidi kuiweka katika hatari ya kushuka daraja African Lyon, ambayo inaburuza mkia, ikiwa na pointi 21 katika michezo yake 28 iliyocheza.

 Yanga bado wanaongoza ligi hiyo wakiwa na pointi 61, katika michezo 25 waliyocheza, huku mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Simba wakiwa nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi 48 katika michezo 19 waliyocheza.

African Lyon:

Douglas Kasembo, Daud Mbweni, Baraka Jafary, Rolland Msonjo, Pato  Ngonyani, Jabir Aziz, Said Mtikila, Hamisi Thabit, Benedictor Jacob, Ramadhan Chombo, Awadh Salum.

Azam FC:

Razack Abarola, Nicholas  Wadada, Bruce Kangwa, Agrey Morris, David Mwantika, Mudhathir Yahya, Salum  Abubakar, Frank Domayo, Obrey Chirwa, Tafadzwa  Kutinyu, Ramadhan Singano.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles