Na BENJAMIN MASESE-MWANZA
SERIKALI imeitaka bodi mpya ya Ushauri ya Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) kuhakikisha inaanzisha utaratibu wa ufugaji nyuki pembezoni mwa hifadhi za taifa ili kuepusha wanyama wasitoroka na kuingia kwenye makazi ya watu.
Imesema ufugaji huo utasaidia Serikali kuhifadhi misitu bila kutumia mitutu ya bunduki kutokana na baadhi ya wananchi kuvamia maeneo hayo sambamba na kupata asali kwa kuwa soko la bidhaa lipo kwa uhakika ndani na nje ya nchi.
Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangala alipokuwa akizindua Bodi mpya ya TFS jijini Mwanza mwishoni mwa wiki.
Alisema ufugaji nyuki itakuwa na manufaa makubwa kwa kila upande ikiwamo ajira na uchumi wa nchi.
Dk. Kigwangala alisema ikiwa asali itakuwapo kwa wingi wawekezaji wa bidhaa zitokanazo na bidhaa hiyo watakuja nchini huku akishauri kuwapo mkakati kababe wa nchi nzima kuwezesha wananchi kwenye ufugaji huo.
“Tumekuwa tukisikia wanyama wanavamia makazi ya watu kila mara na kusababisha vifo na uharibifu wa mashamba, wazo ambalo naliona na nataka TFS mwone kuna umuhimu wa kulifanyia kazi ni kufuga nyuki kwa kuzungukia hifadhi zote za wanyama na misitu.
“Sote tunajua Rais John Magufuli ameagiza kuangalia wale watu wanaoishi karibu na hifadhi tuone namna gani tunawarasimisha ingawa si wote.
“Mchakato huo unaendelea kutembelea maeneo hayo lakini baada maeneo hayo kutenganishwa na kumaliza suala hilo ni vema tukaanzisha ufugaji wa nyuki kwa kuweka mzinga eneo lote.
“Pia tuwashirikishe wananchi hata kwa kuwawezesha nao wafuge kwani soko lipo, ikiwa tutafanikiwa tutakuwa tumepata suluhisho la wanyama kutoroka hifadhini na watu kuvamia misitu yetu.