27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Miundombinu shule za umma iboreshwe

Na LEONARD MANG’OHA

KWA wiki mbili sasa, habari kubwa iliyotawala katika vyombo vya habari pamoja na mitandao ya kijamii, ni kuhusu matokeo ya kidato cha nne kwa mwaka 2018.

Matokeo hayo yaliyotangazwa na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), Dk. Charles Msonde, shule za Serikali hazikufanya vizuri ikilinganishwa na shule binafsi.

Katika vipengele vya shule kumi bora kitaifa, hakukuwa na shule yoyote ya umma, huku katika orodha ya watahiniwa bora kitaifa ilikuwa na mwanafunzi mmoja tu.

Orodha ya wanafunzi bora wa kiume, wanane walitoka shule binafsi huku shule za Serikali zikichukua nafasi mbili, wote wakitoka Shule ya Sekondari Ilboru ya mkoani Arusha. Kwa upande wa watahiniwa bora wa kike shule binafsi zilijitwalia nafasi zote 10.

Kwanza tunapaswa kukubaliana kuwa shule za Serikali hazijafanya vibaya kwa bahati mbaya, kwa sababu mazingira ya shule hizo yanafahamika na wengi.

Ni mazingira ambayo hayawiani kwa namna yoyote na ya shule binafsi kuanzia muindombinu, vitendea kazi, mazingira mazuri ya kufanyia kazi na motisha kwa walimu.

Katika mazingira kama hayo, ni wazi kuwa shule za Serikali haziwezi kushindana na shule za aina hiyo kwa kuzingatia kuwa kwa sasa shule nyingi za vipaji hazipokei tena wanafunzi wa kidato cha kwanza na jukumu hilo kwa kiasi kikubwa limehamishiwa katika shule za kata.

Kwa zaidi ya miaka 13 sasa, shule za kata zimekuwa zikipokea idadi kubwa ya wanafunzi huku zile za vipaji na shule nyingine kongwe zikibaki kuendelea kupokea wanafunzi wa kidato cha sita.

Kutokana na hali hii ni wazi juhudi za ziada zinahitajika ili kunusuru hili kwa kuboresha mazingira ya shule zetu za umma kwa kuhakikisha upatikanaji wa miundombinu rafiki kama vile vyumba vya madarasa na mazingira wezeshi ya kujifunzia na kufundishia.

Tunapaswa kukubaliana japo kwa kutofautiana kuwa mazingira ya shule hizi hayaridhishi, idadi ya wanafunzi katika chumba kimoja ni kubwa na mgawanyo wa walimu ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi hairidhishi.

Endapo shule hizi zitajengewa mazingira wenzeshi kwa kuwekwa vitabu vya kutosha, maabara zenye vifaa muhimu, mabweni na walimu kupewa motisha ni wazi shule hizi zitaongeza ufaulu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles