30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga yaanika ‘uzi’ wa mataji

THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KLABU ya Yanga imezindua jezi mpya zitakazotumiwa na kikosi cha timu hiyo, msimu wa ujao  wa Ligi Kuu Tanzania Bara na mashindano mengine ikiwemo Ligi ya Mabingwa Afrika.

Jezi  za klabu hiyo zilizozinduliwa jana zimetengenezwa na Kampuni ya GSM, iliyoingia nao mkataba wa mwaka mmoja.

Akizungumza wakati wa utambulisho wa jezi hizo jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Yanga, Mshindo Msola, alisema msimu ujao wachezaji wao wataonekana katika jezi zenye rangi ya njano na kijani, bluu na nyeusi.

Alisema rangi za njano na kijani zitawahusu wachezaji wa ndani wakati nyeusi na bluu zitatumiwa na walinda mlando.

Akifafanua zaidi Msola alisema kwa michezo ya nyumbani watatumia jezi za kijani kwa wachezaji wanaocheza ndani, huku kipa wao akivalia jezi ya bluu.

Aliongeza kuwa, kwa mechi za ugenini watatumia rangi ya njano kwa wachezaji wanaocheza ndani na nyeusi kwa mlinda mlango.

“Tulialika kampuni mbali mbali kwa ajili ya kutengeneza jezi lakini GSM wameshinda, tumeingia nao mkataba kwa ajili ya kuwavalisha wachezaji wetu msimu ujao,” alisema.

Alisema wanaamini wataanza msimu vizuri kutokana usajili waliofanya na hasa kwakua umetokana na mapendekezo ya kocha wao, Mwinyi Zahera.


Upande wake, Mkurugenzi wa GSM Hersi Said, alisema watahakikisha wanatengeneza jezi zenye ubora zitakazotumiwa na timu hiyo, baada ya kuingia nayo mkataba wa mwaka mmoja.

“Kuanzia sasa tutafungua duka kubwa litakalokuwa linauza vifaa vyenye nembo ya Yanga, hivyo watu wapata fursa ya kununua vifaa mbali mbali, hata wale mawakala wanaweza kuja kununua kwetu,” alisema.

Naye Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Sport Pesa ambao pia ni wadhamini wa Yanga, Abbas Tarimba, alisema wanajisikia fahari kuwa sehemu ya tamasha la klabu hiyo lililopewa jina la Wiki ya Mwananchi ambalo litafikia kilele kesho.

“SportPesa inafuraha kuwa sehemu ya tamasha hili lijulikanalo kama ‘Sport Pesa Wiki ya Wananchi’, kwani Yanga imeweza kupiga hatua na kubadilisha vitu vingi.

“Naamini katika hali hii itawafanya waweze kuwa na msimu mzuri,” alisema.

Alisema Yanga inachezaji wazuri wanaochipukia akiwemo Paul Godfrey  maarufu pia kwa jina la Boxer .

Katika tukio jingine, baada ya utambulisho wa jezi mpya za klabu hiyo, Tarimba alinunua jezi seti moja kwa Sh.5,00,000.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles