24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga, wanajeshi kazi ipo leo

NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM


TIMU ya Yanga leo itashuka dimbani kusaka pointi tatu dhidi ya JKT Tanzania inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Yanga ipo nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi 32, nyuma ya vinara Azam FC walioko kileleni na  pointi 33.

Miamba hiyo ya soka yenye maskani yao Jangwani jijini Dar es Salaam, imeshuka dimbani mara 12, imeshinda michezo 10 na kutoka sare miwili, huku ikifanikiwa kufunga mabao 21 na kuruhusu mabao saba.

JKT Tanzania yenyewe inakamata nafasi ya sita, ikiwa na pointi 19, baada ya  kushuka dimbani mara 13, ikishinda michezo minne, sare saba na kupoteza miwili.

Kupitia michezo hiyo, JKT Tanzania imefanikiwa kupachika mabao saba na kufungwa sita.

Yanga inaingia uwanjani ikiwa na ari, baada ya kutoka kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Kagera Sugar katika mchezo wao wa mwisho wa ligi hiyo uliochezwa Uwanja wa Kaitaba, mkoani Kagera.

Kwa upande mwingine, JKT Tanzania itakuwa na kiu ya pointi tatu, baada ya kulazimishwa suluhu na Mbeya City katika mchezo wake uliopita uliopigwa Uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Akizungumza na MTANZANIA jana,  Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, Dismas Ten, alisema ukimweka kando winga, Juma Mahadhi, anayesumbuliwa na maumivu ya goti, wachezaji wao waliosalia wapo fiti kuikabili JKT Tanzania.

“Ukimwondoa Mahadhi, wachezaji wengine wako fiti kutumika kadiri mwalimu atakavyoona inafaa,” alisema Ten.

Naye Kocha Mkuu wa JKT Tanzania, Bakari Shime, alisema hana presha yoyote kuelekea mchezo huo, kwani amewaandaa wachezaji wake vema kwa ajili ya kushindana na kushinda.

“Mpira ni mchezo wa makosa, kitu cha muhimu ni kufanya vema katika kila mchezo, jambo la muhimu ni kupata matokeo ya ushindi.

“Kwenye mpira kila kitu kinawezekana, hakuna cha kuhofia, maandalizi yangu kwa Yanga ni ya kawaida na si maalumu,” alisema Shime.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles