27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Wizara yataja Kinondoni kinara ukatili kijinsia

RAMADHAN HASSAN-DODOMA

MKOA wa Kipolisi wa Kinondoni umetajwa kuwa kinara wa ukatili wa kijinsia, jumla ya matukio 2,426 yakitajwa kutokea kwa mwaka 2017.

Hayo yalielezwa jana jijini hapa na Mkurugenzi wa Idara ya Watoto kutoka Idara ya Maendeleo ya Jamii ya  Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mwajuma Magwiza, wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Familia.

Magwiza alikuwa akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Zainabu Chaula.

Alisema taarifa za Jeshi la Polisi kwa mwaka 2017 zinaonesha kuwa mkoa wa kipolisi wenye takwimu kubwa za ukatili ni Kinondoni.

Magwiza alisema jumla ya matukio ya ukatili 13,457 yameripotiwa ukiwemo ukatili wa ngono 3,583 na mimba za utotoni 1,323 kwa mwaka 2017.

Aliitaja mikoa mingine ya kipolisi yenye matukio ya kikatili na idadi ya matukio kwenye mabano kuwa ni Dodoma (1,283), Tanga (1,064), Temeke (984) na Arusha (972).

“Kuongezeka kwa ukosefu wa usawa kunaongeza migogoro katika familia zinazopambana na kuondokana na umasikini.

“Vijana walio kwenye balehe wanaoishi katika kaya masikini mara nyingine wanajiingiza katika hatari nje ya familia zao ili wapate vitu,” alisema Magwiza.

Alisema kwa kipindi cha miezi tisa kuanzia Julai 2018 hadi Machi 2019 jumla ya mashauri ya migogoro ya ndoa yalikuwa 16,832 ikilinganishwa na 13,382 mwaka 2017-2018 ambayo ni sawa na asilimia 34.5.

“Migogoro hiyo sio tu inaathiri ukuaji wa watoto na familia, pia inachangia kurudi nyuma kwa maendeleo ya familia na taifa kwa ujumla,” alisema.

Awali akisoma risala, mwakilishi wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Dodoma, Happy Hiza aliiomba kila familia kuwajibika ili kuondoa lindi la watoto wa mitaani.

Hata hivyo, aliitaka Serikali itumie sheria hasa kwa wazazi na walezi ambao wameshindwa kuwajibika katika malezi.

“Wazazi na walezi tumesahau wajibu wetu, ombi kwa Serikali kila mwanafamilia atimize wajibu wake ili kuondoa watoto wa mitaani, ikishindikana Serikali itumie sheria,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles