24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Wizara ya Afya yaitisha ‘roll call’ ya safari za nje

Dk.Donan-MmbandoNA MAULI MUYENJWA, DAR ES SALAAM

WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imewaagiza wakuu wa vitengo vya wizara hiyo kuwasilisha taarifa za watumishi wake wote waliofanya safari za nje ya nchi baada ya katazo la Rais John Magufuli.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Donan Mmbando, ametoa siku tatu kwa wakuu hao wa idara kumfikishia taarifa hizo ofisini kwake na kuonya kwamba yeyote atakayethubutu kuficha ukweli atachukuliwa hatua.

Dokezo la Mmbando kwenda kwa wakuu wa idara linaeleza kuwa hadi Desemba 21 mwaka huu amri yake iwe imetekelezwa kwa ukamilifu.

“Naagiza wakuu wa Idara ya Rasilimali Watu (DHR), Meneja wa Ulinzi Data (DPM), Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Idara ya Habari, Teknolojia na Mawasiliano (H-ICT), Ofisa Ushirikiano (CO), Wakuu Ofisa Masoko (CMO), Usimamizi eneo la Rasilimali (DAHRM) na Idara ya Huduma kwa Umma (DPS) wanipatie taarifa hiyo kabla ya Desemba 21, mwaka huu,” alisema Mmbando.

Dokezo hilo ambalo gazeti hili limeliona linaelekeza kuwa taarifa zitakazowasilishwa zionyesha nchi ambazo wahusika walikwenda, tarehe walizosafiri, madhumuni ya safari hizo, gharama ya usafiri, aliyezigharimia pamoja na kiasi cha fedha kilichotumika.

Sambamba na hayo, pia anaagiza kuwasilishwa kwa nakala ya kibali cha safari cha Katibu Mkuu kilichomruhusu mtumishi husika kusafiri safari ya nje.

“Taarifa hizo zitajumuisha pamoja na taasisi, hospitali zilizoko chini ya idara zenu,” iliagiza Mmbando.

Rais Magufuli alipiga marufuku watumishi wa umma kusafiri nje ya nchi bila kibali cha Ikulu, ikiwa ni moja ya hatua za kubana matumizi ya fedha za umma.

Tangu kutolewa kwa agizo hilo, watumishi wanne waandamizi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), wamesimamishwa kazi kwa kulikiuka.

Watumishi hao ni Mkurugenzi Elimu kwa Umma, Mary Mosha, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Ekwabi Mujungu, Mkurugenzi wa Uhusiano, Doreen Kapwani na Katibu Muhtasi wa Mkurugenzi Mkuu, Rukia Nikitas, ambao walisafiri nje ya nchi, licha ya kunyimwa kibali cha safari kutoka kwa Rais au Katibu Mkuu Kiongozi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles