24.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 17, 2024

Contact us: [email protected]

Wenje ahoji utekelezaji maazimio ya Bunge

NA MAREGESI PAUL, DODOMA
MBUNGE wa Nyamagana, Ezekiah Wenje (Chadema), amehoji sababu ya ratiba ya Bunge la 18 lililoanza jana mjini hapa, kutoonyesha kama Serikali itawasilisha ripoti ya utekelezaji wa maazimio manane ya Bunge juu ya fedha zilizochotwa katika Akaunti ya Tegeta Escrow iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).
Wenje alitoa kauli hiyo jana baada ya kuomba mwongozo wa spika, akihoji utekelezaji wa maazimio hayo yaliyopendekezwa na Bunge lililopita.
“Mheshimiwa Spika, ukiangalia ratiba ya shughuli za mkutano huu wa 18 wa Bunge, haionyeshi kama Serikali italeta taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge. Kwa maana hiyo, naomba kujua ni lini taarifa hiyo italetwa bungeni hapa,” alisema Wenje.
Akijibu mwongozo huo, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alionyesha kutoridhishwa na uelewa wa wabunge kuhusu kanuni za Bunge kwa kuwa mara kadhaa wanauliza masuala yanayokwenda kinyume na kanuni.
“Waheshimiwa wabunge, kila siku nawaambia muwe mnasoma kanuni kwani inaonekana hamzisomi.
“Kwa mujibu wa kanuni zetu, taarifa hiyo ya maazimio ya Bunge inatakiwa ije bungeni ndani ya miezi 12, na sisi hapa tumebakiwa na miezi 10.
“Kwahiyo, ndiyo maana ratiba yetu haionyeshi kama taarifa hiyo itakuwapo katika mkutano huu,” alisema Spika Makinda.
Sakata la Akaunti ya Tegeta Escrow lilianza kulitikisa Bunge Mei mwaka jana baada ya Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila (NCCR-Mageuzi), kulieleza Bunge jinsi zaidi ya Sh bilioni 300 zilivyochotwa katika akauti hiyo.
Baada ya mjadala mpana bungeni mwishoni mwa mwaka jana, hatimaye wabunge walipitisha maazimio manane wakiitaka Serikali iyatekeleze.
Miongoni mwa mapendekezo hayo ni kuwawajibisha viongozi wa umma waliohusika kwa namna yoyote na uchotwaji wa fedha hizo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles