23.3 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Wengi wamlilia mtangazaji Marin Hassan

 ANDREW MSECHU –DAR ES SALAAM 

RAIS Dk. John Magufuli ameungana na wanafamilia, wafanyakazi wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na wanahabari kuomboleza kifo cha ghafla cha mtangazaji Marin Hassan kilichotokea Dar es Salaam jana. 

Katika salamu zake za rambirambi, Rais Magufuli alisema amepokea kwa mshtuko na masikitiko taarifa za kifo cha ghafla cha mtangazaji huyo mahiri kilichotokea jana asubuhi. 

Alisema alimfahamu Marin kama mtu aliyeipenda sana kazi yake ya utangazaji akiwa mzalendo wa kweli na aliifanya kwa umahiri mkubwa, nguvu na juhudi zake zote kupitia TBC. 

“Ninatoa pole kwa familia, Mkurugenzi na wafanyakazi wote wa TBC, waandishi wote wa habari na wote walioguswa na msiba huu. 

“Ameondoka wakati tunamuhitaji zaidi na naungana na wanafamilia, na wanahabari kumwombea apumzike mahala pema peponi,” alisema Rais Magufuli katika tarifa yake. 

Alisema Marin ni mtu aliyetoa mchango mkubwa katika sekta ya habari na kutangaza kwa ubunifu wa hali ya juu, hasa katika vipindi vya kuelekea Uchaguzui Mkuu na kipindi cha ‘Safari ya Dodoma’ kupitia TBC. 

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBC, Martha Swai alisema wamesikitishwa na kifo cha ghafla cha Marin na kwamba wanatoa pole kwa wanafamilia, wafanyakazi na wote walioguswa na msiba huo. 

Alisema kutokana na taratibu za mazishi, Marin alitarajiwa kuzikwa jana hiyo hiyo nyumbani kwao huko Zanzibar. 

“Kwa hiyo msiba umetokea leo (jana) asubuhi na sasa hivi tunajiandaa kwenda Zanzibar kwa ajili ya mazishi ambayo yanatarajiwa kufanyika jioni ya leo (jana). 

“Tayari utaratibu umeshaandaliwa na ndege maalumu itachukua familia ya Marin pale Dodoma na kuileta Dar es Salaam ambapo pia utaratibu umeandaliwa na itachukuliwa ndege nyingine kwenda Zanzibar kwa ajili ya mazishi leo leo (jana),” alisema Swai. 

Alisema Marin alifariki dunia ghafla jana asubuhi akiwa nyumbani kwake Mbezi Beach, Dar es Salaam na kifo chake kilithibitishwa baada ya kufikishwa katika Hospitali ya Jeshi Lugalo. 

Mkurugenzi wa Matukio wa TBC, Frank Bahati alisema taarifa za awali zilieleza kuwa akiwa nyumbani kwake, Marin alianza kulalamika kuwa hajisikii vizuri majira ya saa 12 asubuhi jana ambapo baadhi ya majirani zake walitaarifiwa na kufika kumsaidia. 

Alisema wakati juhudi za kumsaidia zikiendelea, ilipofika majira ya saa 3 kasoro asubuhi walipata taarifa kuwa amefariki dunia. 

“Wana TBC wamepokea kifo kwa majonzi makubwa kwa sababu jana (juzi) tu saa 3 usiku baada ya kupindi cha ‘TBC Ardhio’, Marin alirejea nyumbani akiwa na baadhi ya watumishi, ambao walimwacha nyumbani kwake nao kurejea makwao. 

“Taarifa hizi zimetustua wote na tunaomba Mungu atupe subira katika kipindi hiki kigumu,” alisema Bahati. 

Baadhi ya watangazaji wenzake wa TBC walieleza kuwa wameshtushwa na kifo hicho kwa kuwa hadi juzi usiku walikuwa pamoja na walifanya mapitio ya kipindi cha ‘TBC Ardhio’ kilichozinduliwa siku tatu zilizopita, kisha kupeana majukumu ya kuanzia asubuhi ya jana. 

Mtangazaji Gabriel Zakaria alisema ni ukweli usiopingika kwamba Marin ana mchango mkubwa sana katika ujenzi wa TBC mpya na kutokana na uwezo na ubunifu wake, wakati wote wamekuwa wakitembea chini ya mawazo yake. 

“Juzi tulizindua kipindi hiki kipya cha ‘TBC Ardhio’ ambacho ni sehemu ya ubunifu wake, kulikuwa na shamrashamra nyingi na alinilisha keki. 

“Kikubwa ni kuwa tutaendeleza yale aliyoyaanzisha na kikubwa zaidi ni kwamba ametangulia mbele za haki, tuendelee kumwombea na zamu yetu ikifika nasi pia tutaungana naye,” alisema Gabriel. 

Alisisitiza kuwa Marin alikuwa ni mtu ambaye alikuwa akiwatia moyo watangazaji vijana na kuwaeleza kuwa wao ndio kina Marin wa kesho na wakati wote alikuwa akiwasisitiza kujitahidi kwa kuwa si kila kitu lazima afanye yeye kwa kuwa kuna wakati ambao hatakuwepo. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles