26.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Waziri Mhagama:Wakamateni wastaafu watakaoghushi nyaraka

UPENDO MOSHA-MOSHI

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama, ameiagiza mifuko ya hifadhi ya jamii nchini, kuwachukulia hatua wastaafu watakaobainika kufanya udanganyifu na kujipatia mafao yasiyo halali.

Waziri Mhagama, alitoa agizo hilo jana wakati wa ziara yake ya kikazi ya siku moja mkoani Kilimanjaro ya kutembelea ofisi za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ya NSSF na PSSSF kwa lengo kuangalia utendaji kazi wa mifuko hiyo.

Katika maelezo yake, Mhagama alisema kwamba, kumekuwa na baadhi ya wastaafu wasiokuwa waaminifu ambao wamekuwa wakifanya udanganyifu katika mifuko hiyo ya hifadhi ya jamii na kujipatia mafao yasiyo halali.

“Pamoja na uwepo wa wastaafu hao, wamekuwa hawachukuliwi hatua zozote za kinidhamu, jambo ambalo limekuwa likisababisha tabia hiyo kuendelea kuwapo.

“Kuanzia sasa, nasema tabia hiyo inapaswa idhibitiwe kwa nguvu zote na uongozi wa mifuko hii, yaani msisite kuwapeleka mahakamani ili iwe fundisho kwa wengine wenye lengo la kufanya wizi wa aina hii.

“Pamoja na hayo, utekelezaji wa agizo hilo uende sambamba na kuimarisha vitengo vya usalama na ulinzi wa mifuko na hatua hiyo itasaidia kuhakikisha wastaafu halali na kuwabaini wastaafu hewa waliotokana na watumishi hewa ili kudhibiti upotevu wa fedha za wanachama,” alisema Mhagama.

Katika hatua nyingine, Waziri Mhagama, aliwaagiza viongozi wa mifuko hiyo kuhakikisha wanabana matumizi ili waweze kumaliza kulipa mafao ya wastaafu.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, William Erio, alisema miongozo yote iliyotelewa na Serikali itafanyiwa kazi sambamba na zoezi la uhakiki ili kudhibiti changamoto ya wizi wa mafao.

Kwa upande wake, Meneja wa NSSF, Mkoa wa Kilimanjaro, Mary Onesmo, alisema mpaka sasa wamefanikiwa kuwalipa mafao wastaafu 4,086 yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 11 na kwamba wengine 42 wanategemea kulipwa mafao yao kabla ya Februari, mwaka huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles