25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

WAZIRI AKERWA UDHAIFU WA UWAJIBIKAJI MAGU

Na BENJAMIN MASESE


MKUU wa Wilaya ya Magu, Khadija Nyembo  amezuia waandishi wasimrekodi  wakati akiomba radhi mbele ya  Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Angelina Mabula.

Ilikuwa ni  baada ya taarifa iliyoandaliwa na maofisa ardhi wa wilaya hiyo  kutupiliwa mbali ikidaiwa kutokuwa na  uhalisia na takwimu za utekelezaji wa maagizo ya Serikali.

Tukio hilo lilitokea  wakati wa ziara ya  Naibu Waziri Mabula  wilayani humo kukagua utekelezaji wa maagizo ya serikali ya  kupima ardhi, kurasimsiha makazi, kukagua mfumo wa ukusanyaji wa kodi ya ardhi sambamba kujua mpango mkakati wa matumizi bora ya ardhi ya jiji na kata.

Akiwa katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya hiyo, Mabula alisomewa taarifa ya idara ya ardhi na Mkuu wa Idara hiyo, Wilfred Mkono.

Taarifa hiyo,   pamoja na mambo mengine, ilikuwa na upungufu mkubwa kiasi kwamba waziri   alikataa kuipokea na kuitupilia mbaya na kuwapa saa kadhaa aandaliwe nyingine.

Mabula alipojaribu kuwahoji baadhi ya   maofisa ardhi juu ya utekelezaji wa maagizo ya Serikali, walionekana kutokuwa na majibu ya msingi ingawa idara   haina  upungufu wa watumishi wala changamoto ambazo zinawazuia kutotekeleza majukumu yao.

Kwa sababu hiyo,  Mkuu wa Wilaya hiyo, Nyembo, alilazimika   kumuomba radhi waziri Mabula huku akimzuia    mwandishi wa Televisheni ya Clouds, Hamza Makuza, kumrekodi.

“Mheshimiwa Naibu waziri, nipende kuchukua fursa hii… aaaha na wewe mwandishi wa Clouds zima kamera yako, zima  sitaki kuonekana kwenye televisheni,”alisema.

Baada ya zuio lake kufanikiwa  alisema:  “Kama navyojua mimi nakaimu wilaya mbili kwa sasa ya Ilemela kule kwako na hapa Magu, isitoshe jana wote tulikuwa huko.

“Naomba nikuhakikishie makosa yaliyojitokeza na maelekezo yako nitasimamia ipasavyo na utapata taarifa nzuri, kama ulivyoelekeza ukitoka Ukerewe utaipitia”.

Awali, Mabula ambaye alizungumza kwa hasira  alisema alisikitishwa na taarifa hiyo kutokuwa na mpango wa mkakati wa matumizi bora ya ardhi, haikuonyesha kuwapo   upimaji na urasimishaji makazi.

Mabula alisema taarifa hiyo haikuwa na takwimu za jumla ya viwanja vilivyopimwa katika vijiji,  idadi ya vijiji vilivyo katika mpango wa matumizi bora ya ardhi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles