31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Wauguzi kizimbani kwa kuondoa dripu

Jiji la Mwanza
Jiji la Mwanza

NA JUDITH NYANGE, MWANZA.

WAUGUZI wawili wa Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana wamepandishwa mahakamani kwa tuhuma za kuomba rushwa kwa wagonjwa pamoja na kuwaondolea mgonjwa matone maji ya dawa maarufu kama dripu.

Akiwasomea shtaka la kwanza mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahamaka ya Mkoa wa Mwanza,  Abeisiza Laurian, Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Lenin Njau alisema watuhumiwa Joyce Mongu na Marystela Winfred wote wakiwa wauguzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nyamagana, walitenda kosa hilo Machi 12, mwaka huu.

Wakili Njau, alisema wauguzi hao huku wakitambua kuwa wao ni watumishi kwa pamoja katika kosa la kwanza waliomba rushwa ya Sh 50,000 kwa Rukia Daudi ambaye ni mzazi wa Amina Steven kama kishawishi cha kumuandaa mgonjwa kwa ajili ya upasuaji wa kujifungua kinyume na taratibu za mwajiri wake.

Katika shtaka la pili linalomkabili mtuhumiwa Marystela Winfred akiwa muuguzi katika hospitali hiyo ya Nyamagana, Machi 12 mwaka huu alidaiwa kupokea Sh 50,000 kutoka kwa Rukia Daudi kama kishawishi ili amfanyie binti yake Amina Steven upasuaji kwa ajili ya kujifungua.

Hata hivyo watuhumiwa walikana mashitaka yote kwa pamoja na wote wawili kulidhaminiwa kwa masharti ya kila mmoja kuwa na mdhamini mmoja atakayesaini hati ya dhamana na Sh milioni 1 na kutimiza masharti ya dhamana hiyo.

Watuhumiwa walikamilisha masharti ya dhamana hiyo na hivyo kuachiwa kwa dhamana, huku kesi hiyo ikipangwa kutajwa tena mahakamani hapo leo.

Kwa upande wake Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mwanza, Mbengwa  Mbuto akitoa ufafanuzi wa kukamatwa kwa wauguzi hao, alisema mnamo Machi 11 mwaka huu muuguzi Joyce alifika wodini alipokuwa amelazwa Amina Steven kwa ajili ya kumfanyia vipimo na baadaye saa 10 usiku alimuagiza muuguzi wa zamu kuomba fedha kwa mgonjwa ili aweze kumhudumiwa.

Machi 12 mwaka huu baada ya ndugu wa mgonjwa kupigiwa simu na wakiombwa Sh 50,000 ili aweze kufanyiwa upasuaji, ndugu wa mgonjwa huyo alifika hospitalini hapo na kwa kuwa hakuwa na kiasi hicho aliomba kuweka simu yake rehani lakini Joyce ambaye ni muuguzi alikataa na kusisitiza kuwa wanahitaji fedha.

Ndugu huyo (jina linahifadhiwa) baada ya kukwama kutoa fedha alishuhudia mgonjwa wake akitolewa dripu kwa maelezo kwamba mpaka atakapolipa kiasi hicho cha fedha alichoombwa, na baadaye kufanikiwa kupata kiasi hicho kwa mkopo na kumkabidhi nesi huyo aliyemrejeshea mgonjwa dripu, lakini muuguzi huyo alipoombwa stakabadhi ya malipo aligoma kutoa.

Alisema katika tukio hilo kiasi kingine cha fedha kilipokelewa kwa M-Pesa na kingine kikiwa ni fedha taslim.

- Advertisement -

Related Articles

3 COMMENTS

  1. This is primitive accomulation of capital,kila sector tz hivi sio mageni ni vya kawaida kabisa,wakuu wa nchi mtusaidie

  2. Wauguzi wenye tabia kama hii wachukuliwe hatua kali za kisheria. Wnanchi pia wawe na ujasiri wa kutoa taarifa kwa vyombo vya sheria ili mambo kama haya yashughulikiwe na yasijirudie tena. Hongera uliyetoa taarifa za kufanya wahusika wakamatwe na kufikishwa katika vyombo vya dola.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles