27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Watumishi hawa sekta ya afya wamulikwe

VITENDO vya udhalilishaji vinavyofanywa na watumishi wa umma kamwe havipaswi kufumbiwa macho.

Tumepata kuandika na kutoa ushauri kuhusu tabia na mwenendo wa baadhi ya watumishi wa afya kukiuka miiko na taratibu za kazi kwa kujihusisha na vitendo vya kinyama na rushwa.

Tunasema kinyama kwa sababu wapo ambao wamekula kiapo cha utii kwenye kazi hii, lakini wamekuwa mstari wa mbele kukivunja kwa tamaa za mwili.

Jambo hili limekuwa likichukua sura mpya kila kukicha katika hospitali nyingi za Serikali.

Pamoja na matukio haya, utasikia mamlaka zinapewa taarifa na kusema hatua za kumsaka zinaendelea. Huu ni ukatili ambao unapaswa kuchukuliwa hatua bila kufumba macho mara moja.

Leo tumelazimika kurudia msimamo wetu wa kutaka wauuguzi wa aina hiyo wachukuliwe hatua ili kurejesha imani kwa wagonjwa wanaokwenda kutibiwa hospitali za Serikali.

Tunasema haya baada ya tukio la kinyama lililotokea Hospitali ya Wilaya ya Igunga mkoani Tabora ambako muuguzi (jina tunalo) amekimbia kituo cha kazi baada ya kudaiwa kumbaka msichana wa miaka 16 ambaye alikuwa mgonjwa.

Huu ni unyama uliopitiliza, haupaswi kufumbiwa macho. Hivi muuguzi huyu aliyepewa dhamana ya kuhudumia wagonjwa anafanya upuuzi huu alafu mamlaka husika zimekaa kimya kitu.  Tena kibaya sasa amekimbia kituo cha kazi na kufutwa kazi na mganga mkuu kwa kushirikiana na jopo lake la wilaya. Lakini husikii wakiomba msaada mamlaka nyingine kuhakikisha wanamkamata na kumfikisha mbele ya sheria ili achukuliwe hatua.

Kibaya zaidi kuna tatizo la magonjwa kama Ukimwi na mengine, haya yote yanafikirisha kwa mtu timamu kubaka mgonjwa ambaye ni mtoto mdogo. Haya yote yamejulikana baada ya Naibu Katibu Mkuu Afya Ofisi ya Rais, Serikali za Mitaa na Tawala za Mikoa (Tamisemi), Dk. Dorothy Gwajima kufanya ziara katika hospitali hiyo na kuelezwa unyama huo na kukithiri kwa vitendo vya rushwa kwa watumishi wa hospitali hiyo.

Dk. Gwajima anapaswa kuchukua hatua bila kupepesa macho katika suala hili ili haki itendeke kwa mgonjwa huyo, mkazi wa Mwanzugi, Mtaa wa Buyumba, Kata ya Igunga Mjini.

Tukio hili limetokea Oktoba 10, mwaka huu saa 4 usiku hadi saa 8 usiku wa kuamkia Oktoba 11.

Kwa kufanya hivi tunaamini itakuwa funzo zuri kwa watumishi ‘mafataki’ ambao wameshindwa kusimamia viapo vya kazi na kujiingiza kwenye tamaa za kimwili.

Lakini tatizo la pili ni kukithiri kwa rushwa ambako mtumishi mwingine (jina tunalo), amefikishwa Mahakama ya Wilaya ya Igunga kwa tuhuma za kudai na kupokea rushwa ya Sh 200,000 kutoka kwa mgonjwa ili amsaidie mama yake kupata dawa za kifua kikuu.

Tunatambua kazi hii inapaswa kufanywa kwa kutoa huduma kwa ari na moyo wa kusaidia wengine. Ndiyo maana tunasema vitendo hivi Serikali isivifumbie macho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles