23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

WATOTO ‘WATUNDU’ HATARINI KUPATA KIFAFA

Veronica Romwald na Cecilia Ngonyani (Tudarco)

WATOTO wenye haraka nyingi (watundu) katika kipindi cha ukuaji wao wapo kwenye hatari ya kupata magonjwa ya akili na kifafa baadaye katika maisha yao.

Hayo yalielezwa hivi karibuni na Mtaalamu wa Tiba ya Utengamao na Mazoezi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Rosemary Kauzeni alipozungumza na MTANZANIA katika mahojiano maalumu.

Alisema wazazi wengi huchukulia kitendo cha mtoto kuwa mwenye haraka nyingi kuwa ni cha kawaida, lakini si kweli bali ni tatizo.

“Ingawa si ugonjwa lakini ni tatizo ambalo linaweza kusababisha  mtoto kupata magonjwa mbalimbali hasa ya  akili na hata kifafa.

“Mara nyingi huwa wana akili nyingi hata hivyo huwa hawawezi kuzitumia,” alisema.

Alisema mara nyingi huwa si watulivu na hawazingatii kujifunza wenyewe huwa waharibifu na   hupendelea kucheza kuliko kujifunza.

“Binadamu ameumbwa kuchangamka, tangu kipindi cha ujauzito, mama huhisi uchangamfu wa mtoto, huweza kumsikia akicheza au hata kuzungukazunguka tumboni mwake,” alisema.

Alisema baada ya kuzaliwa mtoto huendelea kuonyesha uchangamfu wa kulia, kuchezesha miguu na mikono yake kisha huonyesha uchangamfu wa kulia, kufumbua macho, kukaa na hatua nyinginezo wakati wa kukua.

Alisema kazi ambazo mtoto huanza kuzifanya mwenyewe bila kufundishwa na mtu ni kunyonya maziwa ya mama yake.

“Mtoto anapofikisha umri wa miezi minne huanza kuonyesha uchangamfu wa kukaa na kutumia zaidi  mikono yake, sasa mtoto mwenye tatizo huwa hapendi kushika kitu cha aina yoyote,” alisema.

Alisema mtoto mwenye tatizo la haraka nyingi huanza kuonyesha dalili anapofikia hatua ya kukaa chini au kutembea.

“Anakuwa na kasi isiyo ya kawaida, akiwekwa chini tu huanza kuvamia vitu mbalimbali anavyoviona mbele yake,” alisema.

Alisema mara nyingi watoto wenye tatizo hilo hupata ajali mbalimbali ikiwamo za moto.

“Kwa mfano unakuta mama amebandika maji jikoni au ameweka chupa ya chai mezani ghafla anakuta mtoto ameshafika, ameshavunja na tayari ameungua,” alisema.

Aliongeza; “Akiwekwa chini unakuta haraka haraka ameshavamia vitu, wazazi wanaishi kwa wasiwasi wakati wote kumuangalia mtoto wao asipate madhara”.

Alisema ingawa bado hakuna utafiti uliofanywa kubaini ukubwa wa tatizo hilo nchini lakini katika idara hiyo wamekuwa wakipokea watoto wenye tatizo hilo.

“Kwa mfano mwaka 2012 tulipokea watoto 32 katika miezi mitatu ambao walikuwa wameungua moto na tulipozungumza na wazazi wao wengi walidai watoto wao ni watundu sawa na asilimia 10 (si taarifa rasmi),” alisema.

Alisema watoto wengi hufariki dunia kwa kutumbukia kwenye maji na wapo ambao hushindwa kumudu masomo darasani.

“Katika idara yetu tunapokea watoto wengi wenye tatizo hili ambao wanakataliwa shuleni, hawa si ‘slow learners’… wana akili nyingi mno lakini wanashindwa kujifunza kwa sababu ubongo wao una haraka,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles