24.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Watoto, mabinti wenye umri wa miaka 16 -30 wanaongoza kuomba talaka

Na BENJAMIN MASESE- BUNDA

WATOTO na mabinti  wenye umri kati ya miaka 16 hadi 30 katika Wilaya ya Bunda mkoani Mara  wanaongoza kufika katika ofisi za ustawi wa jamii kuomba talaka au kulalamika kutelekezwa na waume zao, imeelezwa.

Pia wakati hali ikiwa hivyo kwa wasichana , takwimu  zilizopo Jeshi la Polisi Wilaya ya Bunda zinaonyesha kuwapo na ongezeko kubwa la watoto kufanyiwa ukatili, vipigo na kutelekezwa  katika kipindi  cha miaka mitatu ya 2016  hadi Juni 2019.

Hayo yalibainishwa na Ofisa Ustawi Wilaya ya Bunda, Fausta Gabriel na Mkuu wa Dawati la Jinsia kutoka Jeshi la  Polisi Wilaya ya  Bunda, CPL Mbijima Julius  katika mikutano ya kampeni ya kupinga ukatili inayotaribiwa na Shirika la Kutetea Wanawake na Watoto la Kivulini.

Akizungumza na wananchi  katika mkutano uliohusisha vijiji vya Mihingo, Manchemweru na Mahanga, Fausta alisema  katika ofisi yake anapokea malalamiko mengi kutoka kwa watoto  na mambinti wenye umri kati ya miaka 16 hadi 30 wakiomba kupewa talaka ili kuachana na waume zao.

Gabriel alisema kwa wiki  moja hupokea   maombi na malalamiko zaidi ya 15 wakitaka talaka na uchunguzi unaonyesha    mabinti  waliingia katika mahusiano ya ndoa wakiwa na umri mdogo.

Aliongeza kuwa mabinti wanaofika katika ofisi yake wengi wao  wanakuwa na wamejifungua watoto zaidi ya watatu.

“Jamani ni suala la masikitiko kidogo ingawa tunaposema nyinyi mnacheka mnaona ni jambo la kawaida lakini tambueni mnatengeneza kizazi na jamii isiyo na ustawi, uchumi, amani na elimu, mfano kwanza hamna mwamko wa kusomesha watoto wa kike badala yake mnawaandaa kuwaozesha.

“Pale ofisini kwangu napokea malalamiko mengi ya watoto na mabinti ambao waliingia kwenye mahusinao ya ndoa wakiwa wadogo, yaani mwoaji na mwolewaji wote walikuwa watoto sasa inafikia hatua kijana akikuwa kidogo anamkimbia mke wake na kuangalia wengine na kutelekeza familia yake.

“Kwa wiki napokea maombi ya talaka na malalamiko ya kutelekezwa na wanaume  zaidi ya 15 hebu fikiria takwimu hiyo kwa mwezi au mwaka inakuaje?, unapotaka kuwakutanisha ili kuwasuluhisha unakuta mume hapatikani, ukiuliza kama wana mali nyumbani unaambiwa hakuna kitu huku tayari mama amezalishwa watoto zaidi ya watatu anatembea nao, hii ni hatari sana,”alisema. Ofisa  huyo alisema  hata watoto wa kike  katika shule za sekondari si wengi ukilinganisha na shule za msingi kwa sababu hawajafikia umri wa kuolewa

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles