33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Watanzania waliobadili uraia kupunguziwa vikwazo

Mindi Kasiga
Mindi Kasiga

Na Jonas Mushi, Dar es Salaam

SERIKALI imesema ina mpango wa kuandaa Sera ya Watanzania waishio nje ya nchi (Diaspora Policy), itakayoainisha namna ya kuwapunguzia masharti  Watanzania waliobadilisha uraia wao ili waweze kuja kuwekeza na kufanya kazi nchini bila vikwazo.

Hayo yalisemwa Dar es Salaam juzi na Ofisa Habari wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa, Mindi Kasiga, alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu kongamano la tatu la Diaspora linalotarajia kuanza leo visiwani Zanzibar.

Alisema hadi sasa Tanzania haijaruhusu uraia wa nchi mbili, sera hiyo itasaidia kuainisha maeneo ambayo yanaweza kuondolewa vikwazo kwa Watanzania waliobadilisha uraia.

“Tunatarajia tukiwa na sera hii, itasaidia kuwaruhusu waliobadilisha uraia kuja kufanya kazi kwa kipindi fulani bila kuwekewa masharti wanayowekewa wageni ambao si Watanzania,” alisema Mindi na kuongeza:

“Tunaweza kuwaruhusu wafanye kazi bila kuwa na kibali cha kazi, lakini pia tunaweza kuwapa haki ya kupata ardhi kwa ajili ya makazi katika kipindi ambacho watakuwa nchini.”

Alisema mabadiliko hayo yatawahamasisha zaidi kuja kufanya kazi na kuwekeza nchini tofauti na ilivyo sasa.

Akizungumzia kuhusu ugumu wa kuruhusu uraia pacha, alisema suala hilo linatakiwa kupitishwa na Bunge, na kwamba hoja iliyopo ni kuhusu usalama wa nchi endapo suala hilo litaruhusiwa.

“Usalama wa nchi ambao umekuwa ukizungumzwa si kuhofia Watanzania waliobadilisha uraia, bali ni wale ambao si raia wa Tanzania ambao watataka kuwa na uraia wa nchi yao na Tanzania,” alisema Mindi.

Alisema kupitia Idara ya Diaspora wanaendelea na jitihada za kuwatambua Watanzania waishio nje na umuhimu wao kwa taifa, ili kuonyesha faida za kuwa na uraia wa nchi mbili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles