25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

WATANZANIA MILIONI 23 HUNYWA MAJI YASIYO SALAMA

Na MWANDISHI WETU

SERIKALI ina kila sababu ya kuangalia kero ya maji nchini na kuitafutia ufumbuzi wa kina ikiwamo kutafuta njia bora ya kuhifadhi bidhaa hii muhimu.

Katika kuadhimisha wiki ya maji duniani, mwaka huu Tanzania iliazimisha siku hiyo kwa kauli mbiu ya “Maji na Maji taka, punguza matumizi na tumia maji yaliyotumika.”

Kauli mbiu hii inatukumbusha na kutuelekeza kuifundisha jamii yetu kuwa upatikanaji wa maji safi ni jambo muhimu katika maisha ya kila siku, hivyo ni muhimu kufanya kila tunaloweza kulinda vyanzo vya maji ikiwa ni pamoja kuyatumia vizuri.

Kwa kutambua umuhimu wa maji pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama, wapo wadau wengine ambao wamekuwa wakiiunga mkono Serikali. Hawa ni pamoja na sekta binafsi, wafadhili na asasi zisizo za kiserikali.

Moja kati ya wadau hao ni Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL). Kampuni hii imetumia zaidi ya Sh bilioni 1.1 kwa ajili ya kuchimba visima 17 katika maeneo mbalimbali nchini tangu mwaka 2010, ikiwa ni jitihada za kupunguza uhaba wa maji. Kupitia programu yake ya ‘Maji ni Uhai, SBL imekuwa ikishirikiana na wadau wengine kuhakikisha Watanzania na hasa wale wanaoishi maeneo yenye uhitaji mkubwa wanapata maji safi na salama.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Uhusiano wa SBL, John Wanyancha SBL inachukulia suala la maji kama moja ya rasilimali muhimu kwa maendeleo ya nchi, ndiyo maana wamekuwa mstari wa mbele kushirikiana na serikali kufanikisha suala hili.

“SBL ina sera inayosisitiza kusaidia maendeleo ya jamii nchini na ‘Maji ni Uhai’ ni moja kati ya vipaumbele vyetu vinne ambavyo vimeelezewa vyema kwenye madhumuni ya kampuni yetu, kusaidia maendeleo ya jamii na kuboresha ustawi wa Watanzania,” anasema Wanyancha.

Mkurugenzi huyo anaeleza malengo mengine kuwa ni pamoja na kutoa ujuzi kwa ajili ya maisha, uhifadhi wa mazingira na kuhamasisha unywaji wa kiasi.

Kwa mujibu wa Shirika la Water Aid, ni asilimia 56 tu ya Watanzania milioni 52 wenye uwezo wa kupata maji kutoka vyanzo salama huku zaidi ya Watanzania milioni 23 wakinywa maji kutoka katika vyanzo visivyo salama.

Maana yake ni kwamba, jamii husika hususan watoto wapo katika hatari ya kupata magonjwa ya mlipuko. Takwimu zinaonesha zaidi ya watoto 3,000 chini ya miaka mitano, wanakufa kila mwaka kutokana na magonjwa ya kuhara yanayoweza kuzuilika yanayotokana na kutotumia maji safi na salama pamoja na matumizi yasiyo sahihi ya vyoo.

Miongoni mwa wadau waliojiunga na SBL kusaidia upatikanaji wa maji ni pamoja na AMREF ambayo kwa kushirikiana na SBL wamesaidia upatikanaji wa maji safi na salama kwenye hospitali ya Mawenzi Moshi, Sekou Toure, Mkamba (Kisarawe-II-Temke, Dar es Salaam), Kata ya Mletele iliyopo Songea, mkoani Ruvuma, Kata ya Pasua Manispaa ya Moshi Wilaya ya Kibaigwa mkoani Dodoma, Katesh (iliyopo Wilaya ya Hanang mkoani Manyara, Makanya na Chang’ombe ‘B’  iliyopo Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam.

“Visima 17 tulivyovichimba maeneo mbalimbali nchini, vimesaidia upatikanaji wa maji safi na salama kwa zaidi ya Watanzania milioni mbili,” anasema.

Kiongozi wa kata ya Chang’ombe, Benjamin Ndalichako anaishukuru SBL kwa kutoa msaada huo wenye manufaa makubwa kwa jamii.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles