31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

WASANII MMEMSIKIA RAIS MAGUFULI?

WENYE kupenda kulalamika, wataendelea kulalamika kuwa sanaa ya Bongo hailipi. Hata hivyo ukiwauliza sababu, watakutajia za ajabuajabu tu.

Wasanii wa kweli, wenye kushughulisha bongo zao, wenye kuzidisha ubunifu, hawalalamiki badala yake wanaendelea kupiga kazi kwa nguvu zaidi. Mafanikio yao yanaonekana.

Kwa mfano hapa Bongo, tunawaona zaidi wasanii wa Bongo Fleva na Bongo Muvi wakichuana kwa upande wa mafanikio na ni kweli kwamba ndio sanaa kuu zaidi kuliko wengine.

Baadhi ya wasanii hao hawana mafanikio, lakini ukichunguza kwa undani utagundua kuwa ni uzembe wao tu na wala siyo kwamba kuna sababu za msingi.

Staa kiwango cha juu katika muziki wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ ni alama tosha ya wasanii wetu hapa nchini, lakini zaidi ni alama ya wasanii wa Bongo Fleva.

Tunaona uwezo wake, namna anavyopambana kutikisa anga za kimataifa. Lakini juzi akiwa live katika Kipindi cha 360 cha Clouds TV, alieleza kuwa miongoni mwa changamoto zinazowakabili ni pamoja na Serikali kuwatupa na kutojali matatizo yao.

Katika kuonyesha kuwa Serikali ya Awamu ya Tano, chini ya Rais John Magufuli ni sikivu, Rais Magufuli alipiga simu live na kuzungumza na mtangazaji Babie Kabae kisha Diamond na kuahidi kushughulikia changamoto hizo.

Rais alikwenda mbali zaidi kwa kuahidi kukutana na wasanii wa sanaa mbalimbali nchini ili kuzungumza nao na kuona namna ya kushughulikia changamoto zinazowakabili.

Hii maana yake nini? Inamaanisha kuwa Serikali inawatambua wasanii, imejipanga kuwasaidia na ina nia ya dhati ya kusikiliza kero zao.

Hapa sasa nimejiridhisha pasi na shaka kuwa wakati Rais Magufuli alipoamua kuunganisha sanaa katika Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo alimaanisha kufanya kitu kikubwa kwa ajili ya wasanii wetu.

Hata utendaji wa waziri wa wizara hiyo, Nape Nnauye unadhihirisha wazi kuwa anatambua thamani ya wasanii na anayo nia ya dhati kuwasaidia wasanii wetu.

Sasa kazi kwenu wasanii kufanya kazi kwa nguvu zaidi, ubunifu zaidi na ubora zaidi, maana Serikali ipo nyuma yenu. Lakini katika kutekeleza hili la kukutana na Rais Magufuli ni vyema kama mngekutana mapema na kupanga agenda za mazungumzo yenu ili mwisho wa siku kuwe na faida ya kukutana meza moja na Rais, badala ya kuishia kupiga naye picha tu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles