Na AVELINE KITOMARY-DAR ES SALAAM
MTAALAMU wa lishe kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MMH), Brenda Maro amewaonya watu wanaotumia njia za kupunguza unene ndani ya muda mfupi kwa kuwa hali hiyo uweza kusababisha madhara katika utendaji kazi wa mwili.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Brenda alisema kuwa ni bora mtu akatumia njia ambazo wataalamu wanashauri kwani zinasaidia mwili kuwa katika hali ya mlingano wa utendaji kazi.
“Lakini hizi ‘diet’ ambazo watu wanapewa baada ya wiki moja mtu anapungua si nzuri kitaalamu, unakuta unausumbua mwili, ndani ya muda mfupi vitu vingine vinakuwa havifanyi kazi kama kawaida, tena unakuta umefanya mabadiliko ya haraka ambayo kwa upande mwingine unaingilia mfumo wa mwili,” alisema Brenda.
Alisema kuwa njia iliyo sahihi katika kupunguza mwili ni kuzingatia mlo kamili na kufanya mazoezi kwani hii husaidia mabadiliko yenye mpangilio mzuri wa mwili.
“Kufaya mazoezi, kuongeza kiwango cha kazi na mazoezi ndiyo yanafanya kilichopo mwilini kitumike ila pia angalia aina ya chakula, unatakiwa kupunguza kiasi cha wanga na kiwango cha vyakula vyenye mafuta katika mlo wako,” alishauri Brenda.
Akizungumza kwa pande wa wanawake ambao wanatoka katika likizo ya uzazi, alisema mara nyingi wanakuwa na tatizo la vitambi ambapo hali hiyo inaweza kuzuilika kwa utaratibu maalumu wa kiafya.
Alisema kuwa wanachotakiwa kufanya ni kula kwa wingi mbogamboga, kuongeza kiwango cha kazi taratibu na kufanya mazoezi kila siku.
“Baada ya kumaliza kipindi cha uzazi kama ni wanga anakula kwa kiasi kidogo tu, hatusemi asile kabisa hapana, apunguze kiasi, ale kiasi kikubwa cha mbogamboga.
“Hatakiwi kwenda kwa ‘speed’ (haraka), anatakiwa kupunguza taratibu kwani miili inatofautiana na asili ni tofauti, viwango vya kupungua vinatofautiana, atapungua tu taratibu, afanye mazoezi, ale mlo kamili kwa wakati, atabadilika siku baada ya siku,” alisema Brenda.