24.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 16, 2024

Contact us: [email protected]

Wanaume wanaofanyiwa tohara kulipwa fidia

Na Mwandishi Wetu
KAMPENI ya tohara kwa wanaume, mashariki na kusini mwa bara la Afrika, inayofadhiliwa na Serikali ya Marekani na Umoja wa Mataifa (UN), imeonyesha mafanikio, licha ya kukosolewa.
Utafiti mpya unaonyesha Marekani sasa inafikiria kubadili sera kwa kuruhusu fidia kulipwa kwa wanaume, ambao watalazimika kukosa kazini wakati wakiuguza majeraha yanayotokana na tohara.
Profesa wa Sera ya Afya ya Usimamizi katika Chuo Kikuu cha North Carolina nchini Marekani, aliliambia gazeti la The East African kwamba Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo, inafuatilia matokeo kutokana na majaribio ya kitabibu, ambayo yeye na watafiti wengine waliyaendesha katika Jimbo la Nyanza nchini Kenya kati ya Juni, 2013 na Februari, 2014.
Utafiti huo, unaonyesha sehemu kubwa ya wanaume 1,500 walioshiriki, walieleza masikitiko yao makubwa kuhusu tohara yalihusu upotevu wa ajira na mishahara wakati wakiuguza vidonda kutokana na tohara.
Hivyo, vocha ya chakula ilitumika katika majaribio ya kulipa fidia kwa wanaume kwa siku moja hadi tatu za mshahara uliopotea.
Makundi matatu ya washiriki wa utafiti huo, yalipokea vocha ya chakula yenye thamani ya Sh 200,700 za Kenya na 1,200, ambapo kundi la nne halikupewa fidia yoyote. Sh 1 ya Kenya ni sawa na Sh 18 za Tanzania.
“Motisha ya kiasi cha Sh 700 au 1,200 za Kenya, iliongeza hamasa ya wanaume kushiriki tohara mara nne hadi sita kulinganisha na makundi ambayo hayakupewa kabisa au yalipewa motisha kidogo,” ulisema utafiti huo wa Profesa Thirumurthy, ambao awali ulichapishwa Agosti 20, 2014, katika Jarida la Chama cha Utabibu Marekani.
Alipoulizwa iwapo viongozi wa kijamii walipinga vocha ya chakula kwa sababu za kimaadili, Profesa Thirumurthy alisema: “Hatukuona upinzani wowote katika suala kama hilo.”
Kwa mujibu wa ofisa mmoja wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani aliyeomba jina lake lisiandikwe gazetini, wakati wizara hiyo ikisema inatambua matokeo ya utafiti kuhusu fidia, haijaonyesha nia ya kurekebisha sera yake ya sasa inayohusu malipo kwa mteja.
Watu zaidi ya milioni 7 walifanyiwa tohara kipindi cha miaka sita nchini Kenya, Rwanda, Tanzania, Uganda na mataifa mengine 10 yaliyolengwa na mpango huo.
Waandaaji wa kampeni hizo, wamelenga kufikia idadi hiyo mara tatu ya kiwango hicho ifikapo mwishoni mwa mwaka, kwa lengo la kupunguza hatari kwa wanaume kuambukizwa virusi vinavyosababisha Ukimwi.
Wanaume 735,000 wa Kenya wengi wao wakitoka kabila la Luo, walifanyiwa tohara kati ya mwaka 2008 na 2013 kupitia programu iliyodhaminiwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) na Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani kwa ajili ya Kukabiliana na Ukimwi (Pepfar).
Kenya, inatarajia kufikia lengo la Serikali la kutahiri wanaume zaidi ya 900,000.
Wanaume karibu milioni 1.3 wa Uganda walitahiriwa katika zahanati zinazosaidiwa na WHO na Pepfar tangu mwanzoni mwa 2014.
Tukio hilo, limeileta Uganda karibu na teluthi moja ya kufikia lengo la tohara milioni 4.2 zinazofanywa kitaalamu.
Tanzania ilifikia karibu nusu ya lengo lake mwishoni mwa 2013 la tohara ya watu milioni 1.4. Rwanda inaburuza mkia kwa majirani zake wa Afrika Mashariki ikiwa na tohara za nyongeza ya watu 281,000. Kiwango hicho ni sawa na asilimia 16 tu ya lengo lililowekwa kwa mujibu ya viwango vya kimataifa.
Pepfar inachangia gharama za kampeni ya tohara kwa kuchangia dola za Marekani milioni 22.1 kwa Tanzania, Uganda dola milioni 21.3, Kenya dola milioni 12.4 na chini ya dola milioni moja nchini Rwanda.
Mamilioni ya dola yanatumiwa na mashirika wakala wa Umoja wa Mataifa katika nchi ambazo wana matumaini ya kuleta ongezeko kubwa la tohara na kupunguza kwa kiwango kikubwa usambaaji wa VVU kwa wanaume.
Uwekezaji huo, ulichochewa na matokeo mazuri ya majaribio yaliyofanyika mwaka 2005 na 2007 huko Kisumu nchini Kenya, Wilaya ya Rakai, Uganda na huko Orange Farm, Afrika Kusini.
Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, tafiti hizo tatu zilizohusisha maelfu ya wanaume wasio na VVU, wenye umri wa miaka 15 hadi 49, zilionyesha tohara ya kitaalamu kwa wanaume ilipunguza kiwango cha usambazaji wa VVU kupitia ngono kutoka kwa wanawake kwenda kwa wanaume kwa karibu asilimia 60.
Lakini tohara kwa wenzi wa wanaume hao haijaonyesha matokeo ya moja kwa moja ya kupunguza hatari kwa wanawake kuambukizwa VVU.
Lakini Georganne Chapin, mkurugenzi wa asasi moja yenye makao makuu mjini New York, Marekani, ambayo inapinga kampeni za tohara kwa wanaume, alihoji sababu za msingi za kuifanya tohara kwa wanaume kuwa njia ya kuwalinda dhidi ya VVU.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles